SUSAN Lyimo, Mbunge Viti Maalum kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ameshinda kura za maoni za kuwania kupitishwa kugombea Ubunge Kinondoni jijini Dar es Salaam katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Lyimo ameshinda katika uchaguzi wa kura za maoni uliofanyika leo Jumatatu tarehe 13 Julai 2020 kwa kuwashinda wenzake watatu.
Mbunge anayemaliza muda wake kwenye jimbo hilo ni Maulud Mtulia wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akitangaza matokeo hayo, Kubra Abdallah, Msimamizi wa Kura za Maoni jimbo la Kinondoni amesema, Lyimo amepata kura 71 sawa na asilimia 62.8 kati ya kura 113 zilizopigwa.
Wengine ni; Moza Ally, Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) aliyepata kura 8, Rose Moshi (30), aliyekuwa diwani viti maalum na Mbezi Mwombeki, Mwenyekiti wa Chadema kata ya Mwananyamala kura (4).
Soma zaidi hapa
Majina matatu ya Lyimo, Rose na Moza yatakwenda kamati kuu kwa uamuzi wa mwisho kupata jina moja litakalopeperusha mbendera ya Chadema kwenye uchaguzi mkuu.
Baada ya matokeo hayo kutangazwa, Lyimo aliwashukuru wajumbe hao, huku akiwaahidi kujipanga ili kushinda katika michakato iliyobaki.
“Niwaahidi, nitafanya kazi bega kwa bega, ninachoomba ni ushirikiano bila ninyi hatuwezi kushinda, tuko pamoja tunajenga Chadema yetu,” amesema Lyimo ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa baraza la wazee wa chama hicho (Bazecha)
“Kama nilivyoahidi nikiwa mbunge, nitafanya kazi kwa bidii kwenye kampeni. Mambo mengine tunaiachia kamati kuu ifanye kazi yake. Nimejipanga kazi kwetu mniombee niweze kufanikiwa,” amesema Lyimo.
Mchakato huo ulianza kwa kuthibitisha akidi ya wajumbe halali wa uchaguzi wa kura za maoni, kisha wagombea wakapata fursa ya kujieleza.
Baada ya shughuli ya kura za maoni kufungwa kwenye majimbo yote, Kamati Kuu ya Chadema itaketi tarehe 30 hadi 31 Julai 2020, kwa ajili ya kuteua wagombea ubunge wa chama hicho, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari mbalimbali
Leave a comment