ANTONY Mavunde, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Ajira na Vijana amesema serikali itaifanyia kazi hoja ya Grace Tendega, Mbunge Viti Maalumu (Chadema), ya kufanya sensa ili kubaini idadi ya vijana wasiokuwa na ajira. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Mavunde ametoa ahadi hiyo jana tarehe 6 Februari 2020 bungeni jijini Dodoma, baada ya Tendega kuitaka serikali kubaini vijana wazurulaji na wanaocheza mchezo wa ‘Pool Table’ wakati wa kazi, kutokana na kukosa ajira.
Naibu Waziri huyo anayeshughulikia masuala ya vijana na ajira, amesema suala hilo litawasilishwa katika Ofisi ya Taifa ya Takwimu, ili ifanyiwe kazi katika sensa ya watu na makazi, itakayofanyika mwaka 2022.
Akizungumzia kuhusu changamoto ya ajira, Mavunde amesema serikali inaendelea kuitatua kupitia njia mbalimbali, ikiwemo kutenga maeneo maalumu ya uzalishaji mali kwa vijana zaidi ya ekari 217,882.36, ambazo zina kidhi shughuli za kilimo, viwanda na biashara ndogo.
Kuboresha mazingira ya uwekezaji hasa katika sekta zinazozalisha nafasi nyingi za ajira, ikiwemo sekta ya kilimo, ufugaji, uvuvi, madini na viwanda.
Pia, Mavunde amesema serikali imeanzisha vituo vya maendeleo ya vijana, majengo ya viwanda pamoja na kuwajengea ujuzi, kupitia programu ya kukuza ujuzi nchini, ili kwa kutumia mafunzo mbalimbali vijana waweze kujiajiri.
“Kwa mwaka huu wa fedha, Serikali inatekeleza mafunzo ya stadi mbalimbali za kazi ambapo jumla ya vijana 49,265 watanufaika, kuweka mazingira bora ya uwekezaji nchini ili kuvutia uwekezaji mkubwa kwenye sekta zenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira hususani kilimo, ufugaji, madini na Viwanda,” amesema Mavunde.
Leave a comment