JOHN Magufuli, Rais wa Tanzania, ametengua agizo la Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe la hakuna kufunga ndoa bila ya cheti cha kuzaliwa, anaandika Hamisi Mguta.
Mwakyembe alitoa kauli hiyo alipokuwa anazungumza na kamati ya ulinzi na usalama, wawakilishi wa wakala wa usajili, ufilisi na udhamini (Rita) jana, mkoani Morogoro, lakini leo Rais Magufuli amefuta maagizo hayo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ikulu na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa, imesema Rais Magufuli amelifuta agizo hilo kwa kigezo kua litanyima haki ya kuoa na kuolewa kwa Watanzania wengi kwa kuwa asilimia kubwa hawana vyeti hivyo.
Kitendo hiko kinaonesha wazi kwamba Waziri Mwakyembe alikurupuka kwenye agizo lake na hakuona kama anaelekea kunyima haki kwa Watanzania.
Rais Magufuli amesema kwenye taarifa hiyo kuwa Serikali haiwezi kuruhusu sharti hilo kutumika kwa kuwa litawanyima haki ya kuoa na kuolewa Watanzania wengi ambao hawana vyeti vya kuzaliwa huku utaratibu wa kupata vyeti hivyo ukiwa unakabiliwa changamoto nyingi kwa wanaohitaji.
“Kwa hiyo ndugu zangu Watanzania msiwe na wasiwasi wowote, endeleeni na utaratibu wetu wa kuoa na kuolewa kama kawaida na kama kuna kifungu chochote cha sheria kinachomlazimisha mtu awe na cheti cha kuzaliwa ndipo aoe ama kuolewa nitamuelekeza Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe apeleke bungeni ikarekebishwe.” Ilieleza taarifa hiyo.
Hata hivyo Rais Magufuli ametoa wito kwa wanasheria kuziangalia vizuri sheria zinazohusiana na kuzwaliwa na kifo na kuoa na kuolewa ili zisileta mkanganyiko kwa wananachi.
Mbali na agizo hilo la Dk. Mwakyembe, Rais Magufuli aliwahi kutengua maagizo mengine kama lile la wakuu wa mikoa, kuwaondoa wafanyabiashara ndogo ndogo ‘Wamachinga’ katika maeneo yasiyo rasmi ambapo rais akataka wafanyabiashara hao kurudi katika maeneo waliyokuwa wakifanya biashara zao.