MUDA mchache baada ya Kangi Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kumtaka Cyprian Musiba, anayejitambulisha kuwa mwanaharakati na mtetezi wa Rais John Magufuli kuacha upotoshaji, naye amemjibu ‘siachi.’ Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Musiba kwenye andiko lake katika ukurasa wake wa twitter leo tarehe 13 Sepemba 2019 amesema, haogopi kukamatwa na kwamba ataendelea.
Amesema, ni miaka mitatu sasa amekuwa akijitambulisha kama mwanaharakati lakini hakuwahi kusema ametumwa na serikali, CCM wala Ikulu.
“Lugola aache kutumia serikali kutaka kunidhibiti kwa sababu ni Waziri. Nimezaliwa siku moja, nitakufa siku moja na hizo jela wameumbiwa watu, kama anataka aje anikamate tu akaniweke. Anataka kuniziba mdomo kisa nimetoa msaada jimboni kwake, sitakubali,” ameandika Musiba.
Mapema leo tarehe 13 Septemba 2019, Lugola alizungumza na wanahabari na kutoa kauli ya onyo dhidi ya Musiba na kumtaka aache uzushi pia kuwadanganya wananchi kwamba uanaharakati wake una baraka za serikali.
Lugola alisema, Musiba amekuwa akichafua watu wakiwemo wanasiasa, wafanyabiashara na viongozi wa umma pamoja na kuwatia hofu.
Pamoja na andiko hilo, Musiba amedai kumshangaa Lugola kwa kuwa naye ni sehmu ya serikali ambayo yeye anaitetea na kuhoji, kwanini anataka kumfunga mdomo.
“Media zangu tunaandika vitu vizuri tu kuhusu serikali, yeye kama sehemu ya serikali sasa anataka kuniziba mdomo kisa nimetoa msaada jimboni kwake, sitakubali na hatoniziba mdomo, hawezi,” amesema Musiba.
Namuomba Kangi Lugola aanze kumsaka Kigogo 2014 ,na Asbert Ngurumo kwanza kutokana na matusi na upotoshaji wake kwa Serikali yetu,badala ya kuniziba mdomo mimi ambaye ni mtetezi wa nchi dhidi ya Vibaraka.Nampenda rais wangu,naipenda nchi yangu . pic.twitter.com/AdwTqazyA6
— UZALENDO WETU (@_uzalendo) September 13, 2019
Leave a comment