MFUMKO wa bei umeongezeka kutoka asilimia 3.2 mwezi Aprili, hadi asilimia 3.5 mwezi Mei mwaka huu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa Irenius Ruyobwa, Mkurugenzi wa shughuli za kitakwimu Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) amesema, kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Mei imeongezeka ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo Aprili mwaka huu.
Amesema, kuongezeka kwa mfumko huo kwa mwezi Mei, kumechangiwa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula kulinganisha na kipindi hiki mwaka 2018.
“Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa mfumko wa bei kwa kipindi hicho ni pamoja na unga wa mahindi, nyama, samaki, matunda, viazi na mihogo mibichi,” alisema Ruyobwa.
Na kuwa, bidhaa zisizo za vyakula zilizochangia ongezeko la mfumko wa bei wa taifa ni mavazi, viatu, mkaa, vyombo vya jikoni, gharama za kumuona daktari hospitaliti za binafsi, dizeli na petroli.
Pia amesema, mfumko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa kipindi cha mwezi Mei, umeongezeka hadi asilimia 2.2 kutoka asilimia 0.9 kwa mwezi April 2019.
Kuhusu hali ya mfumko bei kwa nchi za Afrika Mashariki amesema, Uganda mfumko wa bei kwa mwisho wa mwezi Mei 2019 umepungua hadi asilimia 3.3 kutoka asilimia 3.5 kwa mwezi Aprili mwaka huu.
Kwa upande wa Kenya mfumuko wa bei kwa mwezi Mei, 2019 umepungua hadi asilimia 5.9 kutoka asilimia 6.58 kwa mwezi Aprili mwaka huu.
Leave a comment