UBALOZI wa Ufaransa nchini Tanzania, umefanya makubaliano na Serikali ya Tanzania kuanzisha ushirikiano wa maendeleo ya vijana hususan utoaji wa ajira. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa na Balozi wa Ufaransa, Frederic Clavier mara baada ya kumaliza mazungumzo na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ally, yaliyofanyika makao makuu ya chama hicho jijini Dodoma leo Ijumaa tarehe 11 Desemba 2020.
Balozi Clavier amesema, nchi ya Ufaransa imekubaliana na Serikali ya Tanzania kuwa na ushirikiano wa maendeleo ya vijana hasa upatikanaji wa ajira.
Amesema, maamuzi hayo ni kulenga kuwapatia ajira vijana wapatao milioni nane waliokusudiwa na Serikali.
Balozi Clavier amesema, iwapo vijana watapatiwa ajira wataweza kukuza maarifa ya uzalishaji kwa kupitia vyuo mbalimbali vya ufundi.
Katika makubaliano mengine ni pamoja na kuwa na sauti ya Tanzania katika Jumuiya ya Umoja wa Kimataifa kwa kuzingatia suala la amani.
Katika mazungumzo hayo, Balozi Clavier amesema, Ufaranza imekubari ushughulikiaji wa masuala ya tabia ya nchi kwa kushirikiana na Umoja wa Afrika, Afrika Mashariki pamoja na Umoja wa Mataifa.
Pamoja na mambo mengine, Balozi huyo amesema, Ufaranza imefurahishwa na uanzishwaji wa wizara ya uwekezaji ndani ya Ofisi ya Rais.
Amesema Wizara hiyo inayoongozwa na Waziri, Profesa Kitila Mkumbo, itawezesha uwezeshaji kwa watu binafsi pamoja na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa kuwekewa mazingira mazuri na wezeshi.
Kwa upande wake, Dk. Bashiru amesema, hatua hiyo ni utekelezaji wa Ilani ya chama kilichopo madarakani ya CCM ya mwaka 2020/25.
Dk. Bashiru amesema, Serikali ya Ufaransa imetoa barua ya pongezi kwa Serikali ya Tanzania kwa kumpongeza John Magufuli kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Leave a comment