KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameitaka Serikali itoe elimu kwa vyama vya siasa, kuhusu mkataba wa uwekezaji bandari nchini, ili kuondoa sintofahamu iliyokuwepo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Zitto ametoa wito huo leo Jumanne, jijini Dar es Salaam, akizungumza katika mkutano wa dharura wa Baraza la Vyama vya Siasa, ulioitishwa kwa ajili ya kujadili hali ya siasa nchini.
Mwanasiasa huyo amedai kuwa, sintofahamu iliyokuwepo sasa ndani ya vyama vya siasa kuhusu uwekezaji huo, inatokana na Serikali kutovipa elimu ya kutosha wadau wa vyama vya siasa, kuhusu mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati yake na Serikali ya Dubai, kuhusu uendeshaji bandari nchini.
“Yote haya na mtikisiko uliotokea unaonyesha rangi zetu sisi kuwa sio wamoja tunajificha ficha, suala la bandari limeibua ukali wa maneno. CCM wameitisha kikao chao cha Halmashauri Kuu wamewaeleza wameelewa sasa wanatembea barabarani wanatoa ufafanuzi, lakini tatizo lililopo hakuna usimamizi mzuri wa kisiasa, hamfanyi jukumu lenu la msingi mnaingiza watu kwenye tatizo,” amesema Zitto.
Kauli ya Zitto imetokana na mjadala wa sakata la bandari kuibuliwa ndani ya mkutano huo, ambapo baadhi ya watu walionesha kukasirishwa na baadhi ya vyama vya siasa vinavyotumia lugha zisizo za staha dhidi ya viongozi wa Serikali wakati wanawasilisha hoja zao.
Leave a comment