SERIKIALI ya Mapinduzi Zanzibar imewataka watalii kuzingatia miiko na maadaili ya Mzanzibari hasa katika mavazi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, imewataka wageni na watalii kuzingatia miongozo ya maadili ambayo imekuwa ikitolewa na taasisi zinazosimamia Utalii.
“Wizara inatoa tahadhari kwa wananchi wa Zanzibar, wadau wa utalii na wageni wanaotembeleza Zanzibar kuzingatia maadili na utamaduni wa Kizanzibari, ili kuiepusha na usumbufu wa adhabu za kisheria zitakazochukuliwa dhidi yao,” imeeleza taarifa hiyo.
Imefafanua, katika siku za karibuni kumekuwa na ukiukwaji wa mila, maadili na utamaduni wa Kizanzibari hasa katika suala la mavazi.
“Hali hii hujitokeza kwa baadhi ya wageni na watalii wanaotembelea Zanzibar kwa kushindwa kufuata maadili yanayotaka kuvaa nguo za stara, hasa wanapokuwa kwenye mijumuiko na maeneo mengine ya Umma,” imeeleza taarifa hiyo.
Wizara hiyo mesema jambo hilo si tu limekuwa kero, lakini pia ni kinyume cha sheria za nchi.
Imeeleza, serikali imeonesha kutopendezwa na hali hiyo, hivyo imewasiliana na ofisi za ubalozi za Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika nchi mbalimbali duniani, na kuwapatia machapisho mbalimbali na video fupifupi kuhusu maadili ya utalii ya Zanzibar.
Imeeleza kwamba, lengo la kutoa machapisho hayo ni waziwasilishe kwenye taasisi za nchi wanazoziwakilisha.
Leave a comment