AZIZ Rashid Abdallah (39), mkulima na mkazi wa Mbande Rufu, Mbagala jijini Dar es Salaam anashikiliwa na Jeshi la Polisi, Mkoa wa Kipolisi Temeke kwa madai ya kukutwa na magunia 24 ya bangi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu tarehe 15 Februari 2021, na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke, Amon Kakwale wakati akizungumza na wanahabari jijini humo.
Akielezea tukio hilo, Kamanda Kakwale amesema, mtuhumiwa huyo alikamatwa na bange hizo tarehe 12 Februari 2021, baada ya nyumba yake kukaguliwa na Jeshi la Polisi.
Mbali na magunia ya bange 24 mtuhumiwa huyo anayodaiwa kukamatwa nayo, pia Polisi walimkuta na madebe matatu ya mbegu za bange, magunia 14 ambayo yalikuwa na nusu bange pamoja na fedha taslimu Sh. 2 Milioni.
“Mfanyabiashara huyo katika eneo lake hilo la Mbande Rufu, tulimkamata baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema na tulipofanya upekuzi ndani ya nyumba yake tukamkuta aiwa na magunia 24 ya dawa za kuleya aina ya bangi,” amesema Kamanda Kakwale.
Kamanda Kakwale amesema “Tulimkuta akiwa na nusu ya magunia ya bange 14, anazo mbegu za bangi madebe matatu. Katika muendelezo wa kumpekua na kumhoji tulimkuta na Sh. 2 Mil, ambazo katika mahojiano ya awali alituthibitishia ni kutokana na mauzo anayofanya ya kuuzia wateja wake bangi.”
Kamanda huyo wa Polisi Temeke amesema mtuhumiwa huyo alipohojiwa dawa hizo za kulevya anazitoa wapi, alijibu anazisafirisha kutoka mkoani Morogoro hadi Dar es Salaam, kwa kutumia magari makubwa ya mizigo.
“Jeshi lilitaka kujua bangi hiyo yeye kama mkulima anaipataje, katika mahojiano alituthibitishia aliinunua Morogoro na kufanya utaratibu wa kusafirisha kwa roli la mizigo na kuileta katika maeneo yetu ambapo kwa intelijensia kubwa na ushirikiano wa wananchi tukazikamata,” amesema Kamanda Kakwale.
Leave a comment