KUELEKEA mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga, kikosi cha Yanga kimejipanga kuvunja mwiko ya kutopata matokeo kwenye uwanja huo kwa kipindi cha miaka mitano. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo utapigwa siku ya Alhamisi tarehe 4 Machi 2021, majira ya saa 10 kamili jioni, huku taarifa zikieleza kuwa kikosi cha Yanga kimeshafika jijini humo.
Katika kipindi cha miaka mitano michezo iliyopigwa kwenye uwanja huo wa Mkwakwani ilikuwa ikimalizika kwa sare ya magoli au ya bila kufungana.
Mara ya mwisho Coastal Union kupata ushindi kwenye Uwanja wa Mkwakwani dhidi ya Yanga ilikuwa tarehe 30 Januari 2016 baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.
Kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza uliofanyika Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam, Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 3-0.
Kuelekea mchezo huo ambao unatazamwa na wengi kutokana na Yanga kuwa katika mbio za ubingwa, Afisa Habari wa klabu hiyo Hassan Bumbuli ameeleza kuwa kwenye mchezo huo lazima wapate matokeo na wala hawawezi kukata tamaa.
“Sisi kama viongozi tumepanga kupata matokeo kwenye michezo hii miwili ambayo wengi wanaitolea macho,” alisema Bumbuli.
Afisa habari huo aliongezea kuwa kama viongozi hawawezi kukata tamaa katika kuelekea kusaka taji la ubingwa msimu huu wa 2020/21 ambapo mpaka sasa wapo kileleni mwa msimamo.
“Najua hautujapata maotokeo Mkwakwani toka mwaka 2015 lakini tunakwenda kupata matokeo kwenye mchezo huu bila kipingamzi na hakuna kukata tamaa,” aliongezea Bumbuli.
Leave a comment