DAKIKA 78 zilitosha kuifanya Yanga kuibuka na pointi tatu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Dodoma Jiji, uliochezwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha na kufanya Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 3-1. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa ushindi huo Yanga itakuwa inafikisha pointi 40 baada ya kucheza michezo 16, huku ikiendelea kushika usukani wa Ligi hiyo ambayo imebakisha mchezo mmoja ili kukamilisha duru la kwanza huku Yanga wakiwa hawajapoteza mchezo wowote.
Kwenye mchezo huo Dodoma jiji ilitangulia kupata bao la mapema dakika ya tatu ya mchezo kupitia kwa Seif Karihe baada ya golikipa wa Yanga Metacha Mnata kufanya makosa ya kuutema mpira aliokuwa ameudaka.
Yanga walifanikiwa kusawazisha bao hilo kupitia kwa nahodha wake Lamine Moro kwenye dakika 27 ya mchezo baada ya kuunganisha mpira wa adhabu ndogo na kufanya timu kwenda mapumziko zikiwa zimefungana bao 1-1.
Kipindi cha pili kilianza kwa kocha wa Yanga Cedric Kaze kufanya mabadiliko ya kumuingiza Saidi Ntibazonkiza aliyechukua nafasi ya Michael Sarpong na kufanikiwa kuipatia Yanga bao la pili kwa njia ya faulo kwenye dakika ya 73 mara baada ya kuchezewa madhambi nje ya eneo la hatari.
Dakika tano baadae beki wa kati wa klabu hiyo Bakari Nondo alipachika bao la tatu kwenye dakika ya 78 kwa kuunganisha mpira ulipigwa na Ntibanzokiza.
Gumzo kubwa kwenye mchezo huo alikuwa mshambuliaji Ntibanzokiza aliyeingia kwa mara ya kwanza toka aliposajiliwa na Yanga kwenye dirisha dogo la usajili na kufanikiwa kucheza mechi yake ya kwanza ya kimashindano kwa kufunga bao na kutoa pasi iliyoza goli la tatu.
Leave a comment