HALMASHAURI nchini Tanzania, zimetakiwa kubuni vyanzo vipya vya mapato ya ndani, ili zipate fedha za kutoa huduma kwa wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Alhamisi, tarehe 29 Julai 2021 na Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Ummy Mwalimu, akitoa taarifa ya robo ya mwisho ya mwaka 2020/21, ya mapato ya ndani na matumizi ya Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Majiji, jijini Dodoma.
“Maelekezo ni halmashauri ziendelee kubuni vyanzo vipya vya mapato ya ndani ambavyo haviitakuwa kero kwa wananchi ili kuongeza uwezo wa utoaji huduma kwa wananchi hususani huduma bora za Afya, Elimu na Miudombinu ya Barabara,” amesema Ummy.
Aidha, Ummy ameziagiza halmashauri hizo kuimarisha mifumo ya kielektroniki, ya usimamizi wa ukusanyaji mapato ya ndani
“Halmashauri ziimarishe usimamizi wa ukusanyaji wa mapato ya ndani ikiwa ni pamoja na matumizi ya mifumo ya kielektroniki ya ukusanyaji wa mapato ili kuondoa mianya ya uvujaji wa mapato. kila chanzo kikusanywe kwa kutumia POS machine ili kudhibit upotevu wa mapato ya ndani,” amesema Ummy.
Ummy ameongeza “halmashauri zihakikishe kuwa fedha za makusanyo ya ndani zinazokusanywa zinapelekwa benki ndani ya masaa 24 baada ya kuzikusanya. Ni marufuku na ni kosa la kisheria kwa Halmashauri kutumia fedha zilizokusanywa kabla ya kuzipeleka benki (fedha mbichi) kwa sababu yoyote ile.”
Akitoa taarifa ya mapato hayo, Ummy amesema katika kipindi cha robo mwaka wa 2021/22, halmashauri hizo zimekusanya Sh. 757 bilioni sawa na asilimia 93 ya makisio ya ukusanyaji wa Sh. 814.9 bilioni, kwa mwaka.
Leave a comment