WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro amewataka wadau wa habari nchini kupambana ili kubadili sheria za habari nchini huku akieleza kuwa “wakati ni sasa.” Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Katika hilo, amewataka Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) na Wadau wa Haki ya Kupata Habari (CoRI) kuhakikisha wanatumia vizuri utawala uliopo madarakani kuhakikisha tasnia ya habari inakuwa na sheria nzuri na bora.
Akizungumza na uongozi wa TEF na wajumbe wa CoRI jijini Arusha hivi karibuni, alisema, “kama kuna wakati mzuri wa kulisukuma suala la kubadili sheria za habari, ni sasa.”
“Rais tuliyenaye sasa, (Rais Suluhu Hassan) ameonesha moyo na nia kubwa ya kutetea na kutoa haki za vyombo vya habari na waandishi wa habari nchini.
“Kwa sasa mazingira ni mazuri na yanaruhusu. Lisukumeni suala hili sheria zibadilishwe sasa hivi, maana mkisubiri miaka 10 ijayo, huwezi kujua atakayekuja baada ya hapo atakuwa na mtazamo gani juu ya vyombo vya habari,” alisema Dk. Ndumbaro.
Waziri Ndumaro amemsifu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye kwa kuonesha nia ya kusimamia mabadiliko ya sheria hizo.
Ameahidi yeye na wabunge wengine kushiriki katika kusaidia Tanzania kupata sheria nzuri za habari, kwa kuwa sheria nzuri za habari zitawezesha kukuza haki ya kupata habari, uhuru wa vyombo vya habari na haki ya watu kutoa maoni itakayozalisha maendeleo ya haraka kwa nchi.
TEF na wadau wengine, wanapendekeza mamlaka ya Mkurugenzi wa Idara ya Haabari Melezo ya kufungia vyombo vya habari yafutwe na kiundwe chombo ambacho pamoja na mambo mengine kitashughulikia masuala ya usuluhishi yanapotolewa malalamiko dhidi ya chombo cha habari, badala ya kazi hiyo kufanywa na mtu mmoja.
Sheria nyingine zinazolalamikiwa ni Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Huduma za Posta (EPOCA, 2010), Sheria ya Makosa Mtandaoni (2015), Sheria ya Haki ya Kupata Habari (2016) na Kanuni za Maudhui Mtandao (2018) kama zilivyorekebishwa mara kadhaa.
Leave a comment