WAZIRI wa Afya nchini Tanzania, Dk. Dorothy Gwajima amewaonya watumishi wa afya wanaoiba dawa, wakibainika watafukuzwa kazi pamoja na kunyang’anywa taaluma zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga…(endelea).
Dk. Gwajima ametoa onyo hilo leo Alhamisi tarehe 28 Januari 2021, katika mkutano wa Rais John Magufuli na wananchi wa Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga.
“Kikundi hiki kidogo kinachokwaza watu wengine tutachukua hatua, sio tu za kisheria mahakamani bali mwajiri aliyekuajiri tutamuuliza kama kuna sababu ya wewe kuendelea na ajira,” amesema Dk. Gwajima
“Lakini mabaraza ya kitaaluma, tutayahoji kama kuna sababu ya wewe kuwa mwanataaluma ambaye huna maadili, unaturudisha nyuma,” amesisitiza
Waziri huyo wa afya amesema, hatua hiyo inalenga kupambana na vikundi vya watu wachache wanaoiba dawa za Serikali.
“Kwa pamoja, tukienda hivi tutapambana na hivi vikundi ambavyo vipo, taarifa ninayo, wananchi wanawajua na wananitumia taarifa kwenye simu kila siku,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwajima amesema, Rais Magufuli anajitahidi kuwekeza katika ununuzi wa dawa, lakini changamoto ya uhaba wa dawa katika hospitali za Serikali haiishi kutokana na baadhi ya watumishi wa afya wenye tabia ya udokozi wa dawa.
“Kelele za ukosefu wa dawa zimekuwepo, pamoja na kwamba umewekeza mtaji mkubwa kwenye eneo la dawa, dawa ina mifumo mingi kuanzia kwenye kuzalishwa ambako tumejielekeza huko.”
“Lakini kwenye kuzisambaza hizo dawa na matumizi kwenye vituo husika dawa zinakofika, tumekuwa na changamoto,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwjaima amesema “kwenye maeneo hayo yote, kule kwenye kutumia kumekuwa na kundi cha watu wachache, dawa zimekuwa zinadokolewa, tumeanza mkakati wa kuhakikisha tunawabaini wote hawa na kuchukulia hatua.”
Aidha, Dk. Gwajima amesema, Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, ambao una maoni na changamoto za wananchi kuhusu huduma za afya, utawasilishwa bungeni mwezi Septemba 2021.
“Suala la bima ya afya, kwenye bunge la Septemba tutaingia na muswadsa wa sheria ya bima ya afya kwa wote, ambao utakuwa umehusisha maoni yote na changamoto zote ambazo zipo kwenye eneo hili,” amesema Dk. Gwajima.
Mapema leo Alhamisi, akizungumza katika uzinduzi wa jengo la wagonjwa wa nje katika Hospitali ya Halmashauri ya Kahama mkoani humo, Rais Magufuli alisema Serikali yake itaendelea kuondoa changamoto katika sekta ya afya, ili wananchi wapate huduma bora za afya.
Rais Magufuli alisema Serikali yake imeongeza fedha katika bajeti ya dawa kutoka Sh.31 bilioni hadi Sh. 271 bilioni.
Pia, katika kipindi cha miaka mitano, Serikali yake imeajiri watumishi wa afya 14,000.
Leave a comment