VYOMBO vya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania, imewakamata watuhumiwa 314 wa uhamihaji haramu, ambao watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za kuishi nchini kinyume cha sheria. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi tarehe 28 Januari 2021, Mkuu wa Mkoa huo, Aboubakar Kunenge amesema, operesheni ya pamoja iliyofanywa na vyombo vya ulinzi na usalama Kata ya Mabwepande 24 na 25 Januar1, imewakamata watuhumiwa 314 wa uhamihaji haramu ambapo baada ya kuhojiwa watuhumiwa 84 walibainika ni wahamiaji haramu.
Kunenge amesema, katika watuhumiwa hao 79 wanatokea Burundi, Malawi 02, DRC Kongo 02 na mmoja kutoka Msumbiji ambapo amebainisha watuhumiwa hao wote watafikishwa mahakamani kwa kosa la kuishi nchini kinyume na sheria.
Aidha Kunenge amesema, watuhumiwa wengine 33 bado wanaendelea kuchunguzwa uraia wao huku wengine 197 waliobaki waliachiliwa baada ya kubainika kutokuwa na dosari katika uraia wao.
Hata hivyo, Kunenge amebainisha katika uchunguzi uliofanyika baadhi ya watuhumiwa walibainika kuwa na viashiria vya kujihusisha na uhalifu wa wizi, unyang’anyi, uporaji wa ardhi na kuuza kwa utapeli pamoja na kuzuia wamiliki halali wa ardhi kuingia maeneo yao jambo linalozua migogoro ya ardhi.
Sanjari na hayo, Kunenge amesisitiza utaratibu huo unafanyika kwa kuzingatia sheria na haki za binadamu na watahakikisha hakuna yoyote atakaeonewa ambapo pia, ametoa wito kwa wakazi wa eneo husika kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwafichua wahalifu.
Leave a comment