WATU wawili wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam nchini Tanzania kwa tuhuma za kujifanya maofisa wa usalama wa Taifa, Polisi na Mamalaka ya Mapato Tanzania (TRA), kisha kutapeli Sh.35 milionil. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi tarehe 12 Septemba 2020 na Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Jeshi la Polisi wa Kanda hiyo, wakati anazungumza na wanahabari jijini humo.
Kamanda Mambosasa amesema, mtuhumiwa wa kwanza ni Patrick Tarimo, aliyetapeli Sh.20 milioni kwa raia wa kigeni baada ya kujifanya Afisa Usalama wa Taifa.
“Mtuhumiwa huyo, mnamo tarehe 10 Agosti 2020 alitapeli kiasi hicho cha fedha kutoka kwa raia wa kigeni ambapo alimkamata na kujitambulisha yeye ni afisa usalama wa taifa na kufanikiwa kupata kiasi hicho cha fedha,” amesema Kamanda Mambosasa.
Mtuhumiwa wa pili ni, Castory Wambura, aliyejifanya Ofisa wa Polisi na TRA kisha kutapeli Sh.15 milioni wafanyabiashara watano wa Kariakoo.
“Mnamo tarehe 21 Agosti 2020 mtuhumiwa alitapeli kiasi hicho cha fedha kutoka kwa wafanyabiashara watano ambapo alijitambulisha yeye ni Ofisa wa Polisi na TRA,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa amesema, watuhumiwa wote wanaendelea kuhojiwa na upelelezi utakapokamilika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Leave a comment