RAIA saba wa kigeni wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania kwa tuhuma za uhalifu kwa njia ya mtandao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Watuhumiwa hao ni, Adewale Nuren Oyedes, raia wa Nigeria. Ibrahim Darbey (Liberia), Cream Milton Elias (Liberia), Basube Dominic (DRC), Prince Tito (Liberia), Sibongile Arthur (Afrika Kusini) na Baljit Singh (India).
Akizungumza na wanahabari leo Jumamosi tarehe 12 Septemba 2020 jijini Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Jeshi la Polisi wa kanda hiyo amesema, watuhumiwa hao wamekamatwa nyakati tofauti, baada ya Polisi kufanya msako kati ya kipindi cha Agosti na Septemba 2020.
“Jeshi la Polisi katika maeneo mbalimbali ya Jiji, limefanya msako na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa hawa ambao wamekuwa wakifanya utapeli na wizi kwa njia ya mtandao,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda huyo wa Polisi Dar es Salaam amesema, watuhumiwa hao baada ya kuhojiwa walikiri kujipatia fedha Sh.10 milioni kwa njia ya udanganyifu kupitia njia ya mtandao.
“Baada ya mahojiano walikiri kujipatia kiasi hicho cha fedha ambapo baadhi ya fedha hizo zilitumika kuanzisha duka la vinywaji vya pombe kali maeneo ya Tangi Bovu-Mbezi Beach, walinunua gari Toyota aina ya Mark X, televisheni mbili na magodoro,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa amesema, watuhumiwa hao saba watafikishwa mahakamani hivi karibuni.
Leave a comment