WATANZANIA takribani 300, wamefanikiwa kuondoka salama nchini Ukraine, kufuatia vita iliyoibuka nchini humo baada ya kuvamiwa na Urusi, tarehe 24 Februari 2022. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana Jumanne, tarehe 15 Machi 2022 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula wakati akitaja mafanikio ya wizara yake katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan.
Waziri huyo wa Mambo ya Nje amesema, hadi jana hakuna Mtanzania aliyebaki nchini humo.
“Nafarijika kuwafahamisha kuwa, zoezi la kuwaondoa Watanzania wote waliokuwepo Ukraine wakiwemo wanafunzi limekamilika ambapo hadi sasa takribani Watanzania 300 wamefanikiwa kuondoka na kuelekea nchi jirani na baadhi yao wamerejea nchini,” amesema Balozi Mulamula.
Aidha, Balozi Mulamula amewataka Watanzania waishio nje ya nchi, kujiandikisha katika balozi za Tanzania kwenye nchi walizopo, ili Serikali ijue idadi yao kwa ajili ya kuwasaidia yanapotokea majanga kama hayo.
“Nitoe wito kwa Watanzania wote mliopo nje ya nchi, ni muhimu kujiandikisha katika balozi zetu ili kurahisisha uratibu,” amesema Balozi Mulamula na kuongeza:
“Mimi kama waziri wa mambo ya nje sikujua kama kuna Watanzania wengi sababu kila mmoja ameenda kwa wakati wake. Imekuwa fundishi ni vizuri pale wanapofika waweze kuwasiliana na balozi zetu.”
Leave a comment