WEMA Sepetu, msanii wa filamu na mshindi wa taji la Miss Tanzania 2006 leo ameshindwa kufikishwa katika Mahakama ya Kisutu leo, anaandika Kelvin Mwaipungu.
Wakati Wema akishindwa kuungana na wasanii wenzake 12 waliopandishwa kwenye mahakama hiyo kwa tuhuma za kujihusisha na matumizi ya dawa za kulevya, taarifa za kutounganishwa kwakwe hazijawekwa wazi.
Leo watuhumiwa hao wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa shitaka la utumiaji wa dawa za kulevya.
Hata hivyo, wamepewa dhamana ya Sh. 10 milioni kwa kila mmoja huku wakiwa chini ya uangalizi katika kipindi cha mwaka mmoja.
Baadhi ya waliofikishwa leo mahakamani na kupewa dhamana ni Rommy Jones, Khalid Mohamed ‘TID’, Babuu wa Kitaa, Winfrida Josephat ‘Recho’, Joan Matsein, Hamidu Chambuso ‘Nyandu Tozzy’, Lulu Abbas na Tunda Sabasita.
Baada ya kusomewa kiapo cha mahakama, upande wa Jamhuri uliomba watuhumiwa hao wamrishwe kuwekwa chini ya uangalizi kwa kuripoti polisi mara mbili kwa mwezi kwa kipindi cha miaka miwili ili kuangaliwa kama wameacha tabia ya kutumia dawa hizo hususani bangi.
Ingawa upande wa pili wa utetezi umedai taarifa hizo hazijakamilika wala haizoneshi wanaojihusisha na dawa za kulevya na walikamatwa lini na wapi na hakuna ushahidi wa kujitosheleza wa madai hayo kiasi cha wao kupata dhamana ya kuangaliwa tabia zao bila polisi kutoa ufafanuzi wa kina kwa nini wanahitaji kupata dhamana ya uangalizi wa nidhamu.
Watuhumiwa hao wa matumizi na wauzaji wa dawa za kulevya walitajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda siku ya Alhamisi na kuamuliwa kufika siku ya Ijumaa katika kituo cha kati cha Polisi kwa ajili ya mahojiano kabla ya kupandishwa kizimbani leo.
Leave a comment