Saturday , 25 March 2023
Home Gazeti Habari Mchanganyiko Makonda awavaa Mbowe, Gwajima amkwepa Masogange
Habari MchanganyikoTangulizi

Makonda awavaa Mbowe, Gwajima amkwepa Masogange

Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema na Mbunge wa Hai. Picha ndogo Mchungaji Josephat Gwajima wa Kanisa la Ufufuo na Uzima
Spread the love

PAUL Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, amezindua awamu ya pili ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya ikiwa ni muendelezo wa awamu ya kwanza ambayo alitangaza kuianza wiki moja iliyopita, anaandika Charles William.

Katika awamu ya pili ya operesheni dhidi ya dawa za kulevya katika jiji la Dar es Salaam, Makonda ametangaza majina ya vigogo wakiwemo wanasiasa na wafanyabiashara maarufu hapa nchini.

Freeman Mbowe, Mbunge wa Jimbo la Hai na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Iddi Azzan aliyekuwa Mbunge wa Kinondoni, Yusufu Manji ambaye ni mfanyabiashara na mwenyekiti wa klabu ya Yanga ni miongoni mwa majina makubwa yaliyotajwa na Makonda.

Yumo pia Josephat Gwajima, Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima huku Mwinyi Machapta, akitajwa kama msambazaji mkubwa wa dawa za kulevya katika eneo la Kinondoni ambapo Makonda amesema kijana huyo yupo nchini China kwa sasa.

Jumla ya majina yote yaliyotajwa siku ya leo ni 65 ambapo Makonda amesema miongoni mwa majina hayo wamo wauzaji wa dawa za kulevya, watumiaji pamoja na watu wenye taarifa za wauzaji wa dawa hizo.

“Hawa tunawahitaji siku Ijumaa wiki hii kwaajili ya mahojiano pale Central,” amesema.

Aidha, Makonda amefafanua kuhusu kushikiliwa kwa Francis Cizza @DJ Majizzo ambaye ni mmiliki wa kituo cha redio wa EFM, akisema kuwa mfanyabiashara huyo amekamatwa katika operesheni inayoendelea.

“Mmiliki wa EFM amekwamatwa kulingana na operesheni inayoendelea baada ya kutajwa na vyanzo vyetu vya kuaminika, bado anashikiliwa na uchunguzi dhidi yake unaendelea,” amesema Makonda.

Kuhusu ugumu wa vita anayoiendesha dhidi ya dawa za kulevya jijini Dar es Salaam, Makonda amesema “Vita hii si ngumu. Tumewapa nguvu sana wauzaji wa madawa ya kulevya na kuonekana kama hawagusiki na sasa wanaharibu jamii yetu.”

Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Makonda amekataa kutolea ufafanuzi baadhi ya tuhuma mbalimbali ambazo zimekuwa zikielekezwa kwake na Joseph Kasheku Msukuma, Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini (CCM) ambaye alimshutumu Makonda kwa kuwa na ukwasi wa mali nyingi tofauti na kipato chake.

Msukuma alidai Bungeni jana kuwa Makonda amekarabati ofisi yake kwa Sh. 400 milioni bila kufuata utaratibu wa sheria ya manunuzi, anajenga ghorofa Jijini Mwanza, anamiliki viwanja maeneo mbalimbali pamoja na magari ya kitajiri ndani ya mwaka mmoja tangu awe Mkuu wa Mkoa.

“Hatujadili mambo ya watoto hapa,” amesema kwa kifupi Makonda wakati akijibu swali la mwandishi aliyetaka majibu juu ya tuhuma hizo.

Kuhusu uhusiano wake na Agnes Gerrald @Masogange ambaye anadaiwa kujihusisha na biashara hiyo lakini amekuwa akilindwa na Makonda kwa madai kuwa wana mahusiano ya kimapenzi, Mkuu huyo wa Mkoa amesema tuhuma hizo ni “rasharasha tu.”

“Hizi zingine ni rasharasha tu, mtu ulikuwa wapi kutoa hizo taarifa na kama tumekukamata na tukakuhoji unashindwaje kumtaja kama una ushahidi kuwa anahusika na dawa za kulevya? Kama una taarifa sahihi na za kuaminika zitoe,” amesema Makonda.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Watendaji Kata, Mitaa watakaoshindwa kusimamia usafi kukiona

Spread the love  WATENDAJI wa kata, mitaa na vitongoji na maofisa afya...

Habari Mchanganyiko

Mtia nia urais TLS kukata rufaa kupinga kuenguliwa

Spread the love  MTIA nia ya kugombea Urais wa Chama cha Mawakili...

Habari Mchanganyiko

NBC yazindua kampeni ya mkeka wa ushindi na ATM zake

Spread the loveBENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imetangaza uzinduzi wa kampeni...

Habari Mchanganyiko

Uholanzi wampongeza Rais Samia kuimarisha vyombo vya habari, demokrasia

Spread the love  UBALOZI wa Uholanzi nchini Tanzania, umempongeza Rais Samia Suluhu...

error: Content is protected !!