MABINGWA watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, klabu ya Al Ahly itashuka dimbani hii leo tarehe 16 Februari 2021, dhidi ya El Merreikh ya kutoka Sudan kwenye mchezo wa kundi A, wa michuano hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Al Ahly ambao wapo kundi moja na klabu ya Simba kwenye michuano hiyo wanashuka leo dimbani kwenye mchezo wao wa kwanza mara baada ya kutoka kushiriki michuano ya klabu bingwa dunia ambapo walimaliza kwenye nafasi ya tatu.
Kwenye mchezo huu wa leo Al Ahly ambao wapo chini ya kocha, Pitso Mosimane watakuwa nyumbani kwenye dimba la Borg El Arab uliopo kwenye mjini wa Cairo, nchini Misri.
Mara baada ya mchezo huu wa leo Al Ahly watasafiri kuja Dar es Salaam kwenye mchezo wao dhidi ya Simba utakaopigwa tarehe 23 Februari 2021, kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.
Mpaka sasa Simba ndiyo vinara kwenye kundi hilo baada ya kuibuka na ushindi kwenye mchezo wa kwanza ugenini dhidi ya AS Vita Club kwa bao 1-0, lilofungwa na Chriss Mugalu kwa njia ya penalti.
Leave a comment