SERIKALI ina mpango wa kuanzisha Chama cha Wanasheria walio katika utumishi wa Umma. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mpango huo umeelezwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dk. Adelardus Kilangi katika mkutano wa siku mbili wa Mawakili wa Serikali walio katika utumishi wa umma unaofanyika jijini Dodoma.
Dk. Kilangi wakati akiwasilisha mada kuhusu Nafasi na Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa Mawakili wa Serikali walio katika utumishi wa umma amesema, anakusudia kuanzisha Chama cha Wanasheria walio katika utumishi wa Umma.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali amebainisha kwamba, kuanzishwa kwa Chama hicho ni kwa mujibu wa Ibara ya 74 ya Muswaada wa Sheria ya Marekebisho Mbalimbali ( Na.2) 2018 inayoeleza kuwa , “ Mwanasheria Mkuu wa Serikali anaweza kuanzisha Chama cha Wanasheri katika Utumishi wa Umma”.
Aidha, amesema kuanzishwa kwa chama cha Mawakili wa Serikali walio katika utumishi wa Umma hakutawanyima fursa mawakili hao ya kujiunga au kuwa wanachama wa vyama vingine vya kitaaluma kikiwamo Tanganyika law Society ( TLS).
Kuhusu majukumu ya kuitendaji ya chama hicho, Dk. Kilagi ameeleza kuwa Chama hicho kitakuwa kinakutana mara moja kwa mwaka kwaajili ya kujadili masuala mbalimbali ya kisheria ikiwamo maendeleo ya taaluma hiyo na au kuitishwa na waziri wa katiba na sheria.
Vile vile, amesema Waziri atatunga Kanuni kuhusu usimamizi, uongozi, muundo na uendeshaji wa shughuli za chama pamoja na kupokea ripoti ya mikutano ya chama hicho .
Mawakili hao wa Serikali wapatao mia tisa ( 900) wanatoka Wizara mbalimbali, Idara za Serikali, Taasisi na Mashirika yanayojitegemea, Wakala na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Mkutano huo ambao ni wa pili kufanyikia ulifunguliwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma.
Leave a comment