UONGOZI wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) umewapongeza wanafunzi wanamichezo wa chuo hicho walioshiriki kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Vyuo Vya Elimu ya Juu Tanzania (SHIMIVUTA) kwa kutwaa kombe la ushindi wa kwanza kitaifa kwenye mchezo wa mpira wa kikapu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza kwenye hafla fupi ya kuwapongeza wanafunzi wanamichezo walioshiriki mashindano ya SHIMIVUTA yaliyomalizika hivi karibuni Jijini Mwanza, Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa kitaalamu Prof. Richard Kangalawe ameahidi kuendelea kuwawezesha wanafunzi kwa kuwapatia fursa ya kushiriki mashindano mbalimbali.
Prof. Kangalawe akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa chuo Prof. Shadrack Mwakalila alisema ushindi wa kwanza kitaifa kwenye mchezo wa kikapu ni kitu cha kujivunia na hii itaendelea kuhamasisha wachezaji kujituma zaidi katika mashindano mengine.
Aidha, aliitaja ushindi mwingine ulioletwa na wanamichezo hao kuwa ni pamoja na medali nane kwa wanariadha na michezo mbalimbali.
Kwa upande wake Naibu Mkuu wa Chuo Mipango Fedha na Utawala Dk. Evaristo Haule alisema pamoja na kwamba michezo ni afya lakini ushindi huu umekiheshimisha chuo na kukitangaza.
Aliwataka wanafunzi kutambua namna uongozi unavyowathamini na kuendelea kukua kwenye misingi mema ya maadili kwani ndiyo azma kuu ya chuo.
Hata hivyo, baadhi ya wanafunzi walioshiriki michezo walisema wamefarijika kwa namna chuo kilivyowathamini na kutambua mchango wao na kuahidi ushirikiano wa kutosha kwenye mashindano yajayo huku wakisisitiza wanawake kujitokeza zaidi.
Leave a comment