WAGOMBEA kutoka vyama 12 vya siasa nchini, wamejitokeza kuchukua fomu ya kuwania ubunge katika Jimbo la Singida Mashariki. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Ni baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kutangaza tariba kuanza kuchukua fomu, kurejesha, kuanza kampeni na mwisho wa kampeni na kisha kufanya uchaguzi tarehe 31 Julai 2019.
Chama cha Wananchi (CUF), kimemsimamisha Selemani Ntandu, Masalio Kyara (SAU), Amina Mcheka (AAF), Donald Mwanga (TLP) na Hamidu Hussein (ADA-Tadea).
Wengine ni Ayuni John (UDP), Feruzy Fenezyson (NRA), Maulid Mustafa (ADC), Ameni Npondia (CCK), Abdallah Tumbo (UMD), Amina Ramadhan (DP), Tirubya Mwanga (UPDP).
Mpaka sasa, Miraji Mtaturu ambaye ndio mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), hajajitokeza kuchukua fomu.
Jimbo la Singida Mashariki linatarajiwa kuingia kwenye uchaguzi mdogo baada ya Job Ndugai, Spika wa Bunge kutengua ubunge wa Tundu Lissu kwa madai ya utoro na kushindwa kujaza fomu ya maadili.
Lissu ambaye ni Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, yupo nje ya nchi kwa matibabu baada ya kushambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi tarehe 7 Septemba 2017.
Shambulio hilo lilitokea mchana nyumbani kwake Area D, jijini Dodoma muda mfupi baada ya kutoka kwenye vikao vya Bunge.
Leave a comment