SERIKALI imetangaza ongezeko la wagonjwa wapya 53, wa Homa Kali ya Mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Akitoa taarifa ya ongezeko hilo leo tarehe 17 Aprili 2020 jijini Dar es Salaam, Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, amesema kwa sasa Tanzania ina jumla ya wagonjwa 147 wa COVID-19.
Waziri Ummy amesema wagonjwa wote ni watanzania, ambapo 38 wanatoka jijini Dar es Salaam, 10 visiwani Zanzibar na Kilimanjaro (1), Mwanza (1), Pwani (1), Lindi (1) na Kagera (1).
“Sampuli zilizopimwa katika Maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii jana tarehe 16 na leo tarehe 17 Aprili 2020, zinaonyesha kuwepo kwa watu wapya 53 wenye maambukizi ya Ugonjwa wa COVID-19,” amesema Waziri Ummy.
Pia, Waziri Ummy amesema vifo vilivyotokana na ugonjwa huo vimefikia vitano, huku wagonjwa wanne hali zao zikiwa mbaya, wakati 127 wakiendelea vizuri na matibabu.
Wakati huo huo, Waziri Ummy amesema serikali imesitisha wagonjwa wa COVID-19 kutibiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, badala yake itatumika Hospitali ya Mkoa ya Amana.
“Serikali imeamua hospitali ya Amana kuwa kituo cha matibabu ya COVID-19 ili kuiokoa Muhimbili sababu kuna watu wanahitaji kupata matibabu ya kibingwa ya magonjwa makubwa,” amesema Waziri Ummy.
Leave a comment