MADUKA zaidi ya 400 yako hatarini kufungwa na Halmashauri ya Jiji la Arusha, kutokana na wamiliki wake kushindwa kulipa malimbikizo ya kodi ya pango Sh. 262.5 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Akizungumza na wanahabari jana tarehe 16 Aprili 2020, Anthony Kiwoli, Kaimu Mweka Hazina wa halmashauri hiyo, amesema maduka yatakayofungwa ni ya wafanyabiashara wenye madeni sugu, ambao hawajalipa kodi ya pango katika kipindi cha mwaka mmoja.
Kiwoli amewapa wafanyabaishara hao siku 14 kulipa madeni yao, na kwamba agizo hilo lisipotekelezwa hadi kufikia Mei Mosi mwaka huu, maduka yao yatafungwa.
Amesema siku 14 zimetolewa baada ya viongozi wa wafanyabiashara hao, kuiomba Halmashauri ya Jiji la Arusha kuwapa muda wa kulipa deni hilo.
Maduka yanayotarajiwa kufungwa yako katika eneo la stendi ndogo jijini humo.
Akizungumzia agizo hilo, Loken Masawe, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara mkoani Arusha, amesema kwa sasa anawahamasisha wafanyabiashara hao kulipa madeni yao katika kipindi walichopewa, ili maduka yao yasifungwe.
Masawe amesema wafanyabiashara hao walishindwa kulipa kodi hiyo kwa wakati husika kutokana na biashara kuwa ngumu.
Leave a comment