MWAKILISHI wa kikosi kazi cha Serikali kinachoshughulikia Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote, Bernard Konga amesema katika marekebisho yanayofanywa kwenye muswada huo, maeneo manne kati ya tisa yaliyopendekezwa kufungamanishwa na bima hiyo, yameondolewa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Konga ameyasema hayo leo tarehe 23 Januari 2023 akitoa taarifa ya marekebisho ya muswada huo, yaliyotokana na maoni na mapendekezo ya wadau wa afya, kuhusu kipengele cha ufungamanishaji wa huduma muhimu na bima ya afya kwa wote.
Konga ametaja maeneo yaliyoondolewa kuwa ni, Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN), usajili wa laini za simu, hati za kusafiria (Passport), usajili wa wanafunzi wa kidato cha tano na sita na kitambulisho cha taifa kinachotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
“Tumeondoa suala la usajili laini za simu sababu wengi tumeshasajili kunaweza kusiwe na matokeo makubwa, pia hati ya kusafiria tumeondoa sababu tumekuja kuona kwamba ni haki ya mwananchi kutambuliwa. Tumeondoa usajili wa wanafunzi kidato cha tano na sita sababu Sera ya nchi mwanafunzi asome bure hivyo tunavyoanzisha haya inaonekana tunarudisha nyuma baadhi ya sera,” amesema Konga.
Aidha, Konga ametaja maeneo matano ambayo Serikali inapendekezwa yafungamanishwe na bima ya afya kwa wote, ikiwemo usajili wa wanafunzi wa vyuo vikuu na kati, leseni ya udereva, bima za vyombo vya moto, leseni za biashara na vibali vya kuingia na kuishi nchini (Visa) kwa raia wa kigeni.
Awali, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, amesema katika muswada huo Serikali inapendekeza kufungamanisha baadhi ya huduma na bima ya afya kwa wote, ili kuongeza idadi ya wananchi wanaojiunga kwa hiari kwa lengo la kupunguza mzigo wa ugharamiaji huduma za matibabu.
“Asilimia 99 ya waliokata bima kwa hiari karibu wote wamekata wakiwa wagonjwa, tunaona jinsi Watanzania walivyo na kuifanya bima ya afya kwa wote kuwa lazima, ingawa tumesema ni lazima lakini hakuna kosa la kisheria, hakuna atakayekamatwa wala kufungwa kwa kukosa bima,”amesema Waziri Ummy.
Leave a comment