MKURUGENZI Mtendaji wa Mgodi wa Igalula uliopo Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita, Hussein Makubi ameiomba serikali kupitia Wizara ya Nishati kuwaletea umeme katika mgodi huo ili kuongeza tija ya uzalishaji wa madini ya dhahabu kwenye mkoa huo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Amesema kukosekana kwa umeme katika mgodi huo kumesababisha kushuka kwa uzalishaji wa madini hayo kwani gharama za mafuta yanayotumika kuendeshea mitambo ya uzalishaji ni kubwa ukilinganisha na kupanda kwa bei ya mafuta hayo.
Akizungumza na MwanaHalisi Online jana tarehe 22 Januari, 2023, Mkurugenzi huyo amesema kupatikana kwa nishati hiyo kutaongeza tija kwani wachimbaji wadogo watazalisha zaidi kuliko sasa wanapolazimika kutumia nishati mbadala ya mafuta.
Amesema mbali na mgodi huo wenye takribani ya wafanyakazi zaidi ya 6,000, pia kuna
wachimbaji wadogo ambao pia wanahitaji miundombinu bora ya maji safi na salama, umeme pamoja na barabara ili kurahisisha uendeshaji wa shughuli hizo.
Pamoja na Mambo mengine mkurugenzi huyo amempongeza Waziri wa Madini, Dk. Dotto Biteko kwa usimamizi mzuri wa sekta hiyo na kupunguza tozo mbalimbali ambazo zimefanya wachimbaji kupata nguvu ya kuendelea na shughuli zao na kupata kipato kinachoweza kuendesha maisha yao.
Akizungumzia upande wa utunzaji wa mazingira Mkurugenzi huyo amesema yapo maeneo ambayo ni maalumu kwa shughuli za uchimbaji lakini pia kuna maeneo ndani ya mgodi yameandaliwa kwa ajili ya upandaji wa miti ili kurejesha uoto wa asili.
Leave a comment