ABDALLAH Chikota, mbunge wa Nanyamba (CCM), mkoani Mtwara (CCM), ameiomba Serikali iweke bei elekezi ya zao la korosho katika mfumo wa soko la awali, ili kuondoa changamoto ya viwanda vya ndani kukosa malighafi ya zao hilo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, leo Jumatano tarehe 19 Mei 2021, Chikota amesema wakulima wa zao hilo wanagoma kupeleka korosho kwenye soko hilo, kwa kuwa bei yake haina maslahi.
“Kwa kuwa utaratibu huu wa mfumo wa soko la awali, huwa unakutanisha wenye viwanda na wakulima, lakini hauna ushindani sababu bei ni ndogo na wakulima hawavutiwi kupeleka korosho zao, kama ilivyo kwenye minada mingine ya kawaida,” amesema Chikota.
Chikota amehoji “Je, Serikali ina mpango gani kuweka ‘top up’ kwa bei ile waliyokuja nayo wawekezaji ili kuhakikisha wawekezaji hao wanapata korosho.”
Chikota amesema, changamoto hiyo inasababisha viwanda vingi vya korosho kufanya kazi chini ya uwezo wake, kutokana na kukosa malighafi ya zao hilo kutoka kwa wakulima.
“Takribani viwanda vyote vinafanya kazi chini ya uwezo wake kutokana na changamoto mbalimbali, ikiwemo ukosekanaji wa malighafi sababu hawapati korosho mnadani. Serikali inatoa kauli gani kwa wawekezaji waliofungua viwanda nchini na wale wanaotarajia kufungua?” Amehoji Chikota.
Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji, William Ole Nasha, amesema Serikali itaboresha mfumo huo ili kuwavutia wakulima kuuza korosho zao.
“Kuhusu swali kwamba kuna changamoto korosho kupatikana sababu wakulima hawana imani na mfumo wa soko la awali, nataka nimhakikishie mbunge kwamba, kwa kuwa mfumo umeanza serikali itachukua jitihada kuboresha ili kuweza kuvutia wakulima,” amesema Ole Nasha na kuongeza:
“Tutaboresha ili waone kuwa ile sio kangomba, bali soko lipo lenye lengo kuhakikisha viwanda vya ndani vinapata korosho kwanza kabla ya nje.”
Leave a comment