DAKTARI John Pombe Joseph Magufuli, amewaachia ujumbe Watanzania akiwataka wasitetereke na wamtumaini Mungu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Chato … (endelea).
Dk. Magufuli, aliyekuwa Rais wa tano wa Tanzania, alitoa ujumbe huo, kabla ya mauti kumfika saa 12:00 jioni ya Jumatano tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Ujumbe huo, ulielezwa jana Ijumaa tarehe 26 Machi 2021 na Ngusa Samike, Msemaji wa Familia ya Hayati Magufuli, mara baada ya maziko ya kiongozi huyo.
Maziko hayo yalifanyika nyumbani kwao, Chato mkoani Geita na kuhudhuliwa na maelfu ya waombolezaji akiwemo, Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli.
Mara baada ya maziko hayo, Samike akitoa salamu za shukrani kwa waombolezaji akisema, Dk. Magufuli kabla ya mauti kumfika, alitoa maombi matatu “aliyotoa asubuhi hiyo lakini ni mawili tu ambayo familia inayakumbuka.”
Aliyataja maombi hayo kuwa ni, Watanzania wasitetereke bali wamtegemee Mungu katika kila kitu.
“Ni maombi mawili tu familia inayakumbuka, la kwanza aliwaombea Watanzania wasitetereke na wamtegemee Mungu kwani ni muweza wa yote na hakuna anayemtegea asiweze kufanikiwa.”
“La pili aliwaombea viongozi wa dini zote wasiyumbishwe katika imani zao na wazidi kumuomba Mungu,” alisema Samike.
Kiongiozi huyo, amewatumikia Watanzana kwa nafasi ya urais kwa kipindi cha miaka mitano na miezi mitano, kuanzia tarehe 5 Novemba 2015 hadi 17 Machi 2021, alipofariki dunia akiwa madarakani.
Hayati Magufuli, hadi anafikwa na mauti, ameacha watoto saba ambao ni Suzana, Edna, Mbalu, Joseph, Jesca, Yuden na Jeremiah.
Pia, ameacha Mjane Janeth, ambaye walifunga ndoa takatifu Kanisa Katoliki la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), mwaka 1989.
Leave a comment