MWENYEKITI wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema tangu kuanzishwa kwa Tume hiyo, sekta ya madini imeendelea kuimarika kutokana na mafanikio yaliyopatikana ndani ya muda mfupi ikiwa ni pamoja na kasi ya ukusanyaji wa maduhuli, uanzishwaji wa masoko na vituo vya ununuzi wa madini nchini na utoaji wa leseni za madini.
Amesema tangu kuanzishwa kwa Tume ukusanyaji wa maduhuli umepanda kutoka Sh bilioni 346.78 kwa kipindi cha mwaka 2018-2019 hadi kufikia Sh bilioni 624.61 kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2021-2022 ikiwa ni sawa na asilimia 96.09 ya lengo la mwaka husika. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Profesa Kikula ameyasema hayo leo tarehe 11 Oktoba, 2022 jijini Mwanza kwenye kikao cha Tume ya Madini kilichoshirikisha Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Mhandisi Yahya Samamba, Wakurugenzi, Mameneja na Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa.
Kikao hicho kimelenga kujadili namna ya kuboresha utendaji kazi hasa kwenye eneo la ukusanyaji wa maduhuli kwa mwaka wa fedha 2022-2023, usimamizi wa masoko na vituo vya ununuzi wa madini, usimamizi wa mazingira na afya kwenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini na namna watanzania wanavyoweza kunufaika kupitia sekta ya madini.
Profesa Kikula ameeleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa masoko 42 na vituo vya ununuzi wa madini 83 na ongezeko la utoaji wa leseni za madini.
Pia katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021-2022, Tume ilitoa jumla ya leseni za madini 9,498 ikilinganishwa na leseni 6,314 zilizotolewa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020-2021.
Aidha, Profesa Kikula amesema ili kusogeza huduma karibu zaidi na wadau wa madini, Tume ilianzisha ofisi mpya za madini katika mikoa ya Mbogwe na Mahenge.
Ameongeza kuwa mchango wa sekta ya madini kwenye Pato la Taifa umeendelea kukua kutoka asilimia 4.8 katika kipindi cha mwaka 2018 hadi kufikia asilimia 7.2 katika kipindi cha mwaka 2021.
Leave a comment