KUTOKANA na juhudi za uhifadhi wa mazingira, Wilaya ya Gairo kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) mwaka jana imefanikiwa kuvuna tani moja za asali kutoka katika mizinga 82. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yameelezwa jana tarehe 8 Machi, 2022 na Mhifadhi mkuu wa Misitu wilaya ya Gairo, Robert Mwangosi wakati akielezea mikakati ya wilaya hiyo katika ufugaji wa nyuki.
Amesema Gairo inafanya vizuri katika uzalishaji wa asali ndio maana TFS imejikita katika kuwahamasisha na kuwaelimisha wananchi juu ya ufugaji wa nyuki.
“Asali ya Gairo inakubalika vizuri katika soko… ina sifa ya kuganda kutokana na mimea ya maeneo haya na mimea tunayoendelea kuipanda. Tuna mimea inayoitwa ‘akeshia’ ambayo maua yake ndio yanayopelekea asali hiyo kuganda.
“Pia ubora wa asali umesababisha kupata wateja wengi nje ya Gairo ndio tunahamasisha wananchi kupanda miti na kuangalia aina ya mimea ambayo inafanya vizuri na inayopendwa na nyuki. Hii itawawezesha kuongeza uzalishaji wa asali,” amesema.
Naye Afisa ufugaji nyuki – TFS Gairo, Aled Heneriko amesema msimu huu wa mvua ni msimu wa nyuki kujenga hivyo muda wa kuisafisha mizinga iliyokuwa michafu.
“Mizinga ikiwa misafi makundi ya nyuki yatahama kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine yataingia kwenye mizinga hiyo na kutuwezesha kupata mazao mbalimbali,” amesema.
Leave a comment