MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deudatus Balile, ameshauri Sheria ya Huduma ya Vyombo vya Habari ya 2016, irekebishwe ile iwe na kifungu kinachotoa adhabu kwa kampuni zitakazoshindwa kulipa fedha za matangazo kwa vyombo ya habari.Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo wa Balile, umetolewa leo Alhamisi, tarehe 2 Juni 2022, akizungumza katika mafunzo ya sheria za habari Tanzani kwa wanahabari, yaliyofanyika mtandaoni.
Balile amesema, kukiwa na utaratibu wa kutoa adhabu kwa kampuni zinazoshindwa kulipa fedha za matangazo bila sababu za msingi, itasaidia kutokomeza malimbikizo ya madeni ya matangazo kwa vyombo vya habari, kitendo kinachopelekea vyombo hivyo kukosa fedha za kujiendesha.
“Kuwe na kifungu cha kuwapeleka jela miezi kampuni zisizolipia matangazo ya vyombo vya habari, naamimi mkurugenzi wa taasisi akisikia taasisi nyingine imefikishwa mahakamani kwa kutokulipa, atalipa kwa wakati,” amesema Balile.
Katika hatua nyingine, Balile ameshauri sheria hiyo ifanyiwe marekebisho, katika kifungu kinachompa mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo, kuwa mratibu wa matangazo ya wizara, mashirika na taasisi za serikali , kwenda katika vyombo vya habari ili kuondoa urasimu.
“Sheria hii inataka matangazo yapitie kwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo. Mkimpa majukumu mkurugenzi kutakuwepo urasimu. Tunaomba kifungu hiki kifutwe ili mkurugenzi asitoe matangazo,” amesema Balile.
Aidha, Balile, ameshauri sheria hiyo irekebishwe ili kuwezesha raia wa kigeni kumiliki vyombo vya habari ili kuongeza ufanisi wake ikiwemo kwenye suala la rasilimali fedha.
“Kuna kitu watu wanadhani kwamba wageni kumiliki vyombo vya habari ni hatari kwa kuwa vinamilikiwa na mtu ambaye hawawezi kumdhibiti au sio mzalendo. Dhana hii sio sahihi sababu kampuni nyingi zinamilikiwa na raia wa kigeni kwa kushirikiana na Watanzania na zinafanya vizuri,” amesema Balile na kuongeza:
“Ikiwa sheria inaruhusu wawekezaji kutoka nje kumiliki kampuni za simu kwa asilimia 100, mwekezaji yeyote kutoka nje anayetaka kumiliki kampuni ya habari kwa asilimia 100 aruhusiwe kufanya hivyo. Kwa sasa mwekezaji kutoka nje haruhusiwi kumiliki zaidi ya asilimia 49.”
Leave a comment