MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), imetangaza kuanza kufanya uchunguzi tukio la raia wa kigeni kuwinda mamba mwenye ukubwa unaodaiwa kuweka rekodi ya dunia, ili kubaini kama kulikuwa na ukiukwaji wa sheria au lah!. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo ilitolewa jana tarehe 27 Disemba 2023 na Afisa Habari wa Kitengo cha Uhusiano na Umma TAWA, Beatus Maganja, baada ya video fupi inayomuonyesha mzungu huyo akiwa na mamba baada ya kumuwinda, kusambaa kwenye mitandao ya kijamii.
“Kuhusu video inayosambaa, TAWA inaendelea na uchunguzi kuona kama kuna ukiukwaji wa sheria za uwindaji. Mara baada ya uchunguzi kukamilika taarifa kamili itatolewa na hatua za kisheria zitachukuliwa iwapo ukiukwaji utabainika,” imesema taarifa hiyo.
Aidha, taarifa hiyo imesema uwindaji wa kitalii hufanyika kwa kuzingatia Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Sura ya 283 pamoja na kanuni za uwindaji wa kitalii za 2015 na marekebisho yake. Pia, husimamiwa na Mkataba wa Kimataifa wa Biashara ya Wanyamapori na Mimea iliyohatarini kutoweka (CITES), ambayo Tanzania imeridhia.
“Mamba ni miongoni mwa wanyamapori wanaolindwa na mikataba hii na wamewekwa katika kundi la pili ambalo linaruhusu matumizi ya uvunaji ikiwemo uwindaji wa kitalii,” imesema taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, sheria zinaruhusu mamba wanaowindwa kutozidi idadi ya 1,600 kwa mwaka, wenye urefu usiopungua sentimita 300, wenye vibandiko maalum vinavyofungwa katika ngozi kuonesha wanawindwa na vibali vya CITES vinavyotumika kusafirisha nyara zake.
“Chini ya sheria ya mkataba huo, mtu yeyote anaruhusiwa kufanya uwindaji wa kitalii baada ya kupata kibali kutoka TAWA na kutimiza masharti kama ilivyobainishwa hapo juu. TAWA inawajibu wa kusimamia uwindaji huo katika hatua zake zote,” imesema taarifa hiyo.
Baada ya video hiyo kusambaa baadhi ya watu walikosoa wakidai kitendo hicho ni ukiukwaji wa sheria na kwamba kama angefanya mtanzania angechukuliwa hatua haraka.
Leave a comment