Friday , 26 April 2024
Home Habari Mchanganyiko Tanzania yasaka mwarobaini ukataji holela misitu
Habari Mchanganyiko

Tanzania yasaka mwarobaini ukataji holela misitu

Spread the love

 

SERIKALI ya Tanzania, imetoa wito kwa wasomi, watafiti pamoja na wafanyabiashara wa nishati mbadala, kutafuta njia zitakazowawezesha wananchi kuachana na matumizi ya kuni na mkaa, ili kutokomeza tatizo la ukataji holela miti katika misitu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Wito huo umetolewa leo Jumamosi, tarehe 5 Juni 2021 na Makamu wa Rais, Dk. Phillip Mpango, katika sherehe za maadhimisho ya siku ya mazingira duniani, zilizofanyika jijini Dodoma.

“Napenda kutoka wito kwa wafanyabiashara hasa wa gesi ya kupikia nyumbani na wadau wengine, waweze kubuni mbinu za kusaidia wananchi wa kipato cha chini, waweze kumudu gharama za nishati mbadala,” amesema Dk. Mpango.

Wakati huo huo, Dk. Mpango amewataka wadau wa nishati mbadala, kubuni miradi itakayoongeza matumizi ya nishati mbadala nchini, ili kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, yanayosababisha misitu kupotea kutokana na miti kukatwa.

Dk. Philip Mpango, Makamu wa Rais wa Tanzania

“Wadau hatuna budi kuongeza nguvu kutekeleza miradi inayolenga kuongeza matumizi ya nishati mbadala, ikiwemo gesi asilia na vifaa vinavyotumia nishati kidogo katika kupika,” amesema Dk. Mpango.

Aidha, Dk. Mpango amesema Serikali itapitia upya viwango vya kodi kwa wafanyabaishara na wazalishaji wa nishati mbadala ikiwemo, gesi asilia, ili kupunguza gharama za uzalishaji kwa ajili ya kuondolea mwananchi mzigo wa gharama za kupata nishati hizo.

“Tatizo kubwa kwetu ni namna gani tunapunguza bei ya nishati mbadala na bei ya jiko, niwasihi vyuo vyetu na watafiti wengine wafanye kazi kutafiti, kwa nini bei ya nishati mbadala inakuwa kubwa,”

“ Na nini kifanyike, kama kuangalia mfumo wa kodi tuutazame, lakini kama gharama ya kuzalisha nishati mbadala nazo ziweze kutazamwa,” amesema Dk. Mpango.

Makamu huyo wa Rais wa Tanzania, amesema matumizi ya kuni na mkaa katika shughuli za nyumbani na kwenye biashara, yanaendelea kuongezeka siku hadi siku, kutokana na ongezeko la idadi ya watu.

Moja ya misitu iliyopo Tanzania

Na kwamba, tafiti za mapato na matumizi ya kaya binafsi zilizofanywa kuanzia mwaka 2007 hadi 2018, zinaonesha katika kila kaya 100, 90 zinatumia kuni na mkaa kama nishati ya kupikia.

Amesema ongezeko la matumizi hayo, limesababisha vitendo vya ukataji miti kuongezeka, ambapo mkoa wa Dar es Salaam peke yake, unatumia heka 188 za misitu kila mwaka, kwa ajili ya kupata kuni na mkaa.

“Mfano Dar es Salaam wanatumia zaidi ya magunia 500,000 ya mkaa, kwa mwaka mmoja, sawa na tani 45,000, mita za ujazo wa miti 75,000. Kwa lugha nyepesi sawa na kukata heka 188 kila mwaka,” amesema Dk. Mpango na kuongeza:

“Hali hii kwa kweli inatia wasiwasi, maana imeanza kusababisha kupotea misitu yetu kwa haraka na kuvurugika mifumo ya ikolojia na hivyo kuongeza kasi ya kuenea hali ya jangwa na ukame katika nchi yetu.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Wakili: Ukimpa zawadi mwenza marufuku kumpora hata mkiachana

Spread the love  WANANDOA na watu waliko kwenye mahusiano ya kimapenzi, wamekumbushwa...

Habari Mchanganyiko

Majaliwa: Mvua zimesababisha vifo vya watu 155, kuendelea hadi Mei

Spread the love  WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema mvua kubwa za El-Nino...

Habari Mchanganyiko

Exim Bank yatoa  vitanda kwa shule ya Jeshi la Polisi Moshi

Spread the love  BENKI ya Exim imekabidhii  seti ya vitanda kwa Shule...

Habari Mchanganyiko

NBC yakabidhi vitanda Shule ya Polisi Moshi

Spread the loveBenki ya NBC imekabidhi msaada wa vitanda 28 kwa Shule...

error: Content is protected !!