SERIKALI ya Tanzania, iko mbioni kuzindua nembo maalumu itakayotambulisha bidhaa zinazotengenezwa nchini, pamoja na mfumo wa kusambaza taarifa za biashara nchini humo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 5 Julai 2021 na Waziri wa Viwanda na Biashara, Prof. Kitila Mkumbo, katika ufunguzi wa maonesho ya 45 ya kimataifa ya biashara ‘Sabasaba’, mkoani Dar es Salaam. Maonesho hayo yamefunguliwa na Makamu wa Rais, Dk. Phillip Mpango.
“Katika maonesho ya miaka 45, tumepanga kuzindua huduma na bidhaa mbalimbali mpya katika sekta ya viwanda, kwanza tutazindua nembo maalumu itakayotambulisha bidhaa za viungo vinavyozalishwa nchini,” amesema Prof. Mkumbo.
Prof. Mkumbo amesema, huduma hizo zitazinduliwa katika maonesho hayo na kwamba uzinduzi wa mfumo wa usambazaji taarifa za biashara, utafanywa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Faustine Ndugulile.
“Pili, tutazindua mfumo maalumu wa kusambaza taarifa za biashara, utakaowezesha kufahamu fursa na taratibu za kufanya biashara nchini,” amesema Prof. Mkumbo.
Pia, Prof. Mkumbo amesema, katika maonesho hayo kutafanyika uzinduzi wa duka la kidigitali.
“Tatu, tutazindua mfumo wa duka la kidigitali, utafanywa na Dk. Ndugulile katika maonesho haya,” amesema Prof. Mkumbo.
Leave a comment