NAIBU Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI Dk. Festo Dugange amesema serikali itachukua hatua za kumsimamisha kazi Meneja wa TARURA Wilaya ya Karatu kama atashindwa kusimamia ujenzi wa barabara yenye urefu wa mita 900 kwa kiwango cha lami iliyopo wilayani humo. Anaripoti Mwandishi, Arusha … (endelea).
Dk. Dugange ametoa kauli hiyo jana tarehe 20 Januari, 2022 wakati akikagua barabara hiyo.
Amesema kumekuwepo na malalamiko mengi dhidi ya mkandarasi Bonas and Herbert Enterprises Limited kwa kushindwa kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo ambayo ni ahadi ya aliyekuwa Rais wa awamu ya tano, Hayati Dk. John Magufuli mwaka 2019/2020.
Amesema barabara hiyo imekuwa kero kwa wakazi wa Karatu kwani kutokana na ubovu wake kumetokea ajali za mara kwa mara hususani waendesha pikipiki.
Aidha, ameeleza kutofurahishwa na utendaji wa Meneja wa TARURA wilaya ya Karatu kwa kuwa amefanya uzembe katika kusimamia barabara hiyo kama vile kuweka vifusi barabarani kwa muda wa siku 90 bila kufanya lolote wakati wananchi wanapata shida.
“Ifikapo tarehe 28/02/2022 barabara hii lazima iwe imekamilika kwa viwango vinavyokubalika, vinginevyo Meneja wa TARURA utakuwa hautoshi kuwa Meneja wa TARURA sehemu yoyote, utaenda kufanya kazi nyingine” alisema Dk. Dugange.
Naye Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Karatu, Mhandisi Kheri Mchele amesema wamejipanga kumsimamia kikamilifu mkandarasi huyo.
Kwa upande wake Msimamizi wa Mkandarasi Bonas and Herbert Enterprises Limited, Sifuni Mlacha amesema changamoto ya kulipwa fedha ilisababisha kusimama kwa ujenzi huo lakini baada ya kulipwa fedha zao watakamilisha ujenzi huo kwa wakati.
Barabara hiyo inayojengwa kwa kiwango cha lami ina thamani ya shilingi milioni 500 na imegawanyika sehemu tatu ambazo ni Mahaka hadi TRA mita 230, NBC hadi Kudu mita 150 na Tarafa hadi Alimpya mita 520.
Leave a comment