BAADHI ya mambo yaliyofanywa na Marehemu Dk. Reginald Abraham Mengi ambayo hayajulikani kwa ukubwa wake, yameelezwa na Job Ndugai, Spika wa Bunge. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Leo tarehe 3 Mei 2019 bungeni jijini Dodoma, Spika Ndugai ametumia dakika kadhaa kueleza sifa na kazi zilizofanywa na Dk. Mengi katika uhai wake kwa manufaa ya taifa.
Miongoni mwa hayo ni uchangiaji wa kiasi cha Sh. 50 milioni katika mradi wa kujenga vyoo vya mfano kwa watoto wa kike katika majimbo yote ya Tanzania.
Amesema, Dk. Mengi ambaye alifariki dunia usiku wa kuamkia tarehe 2 Mei 2019, Dubai, Umoja wa Falme ya Kiarabu (UAE).
Kabla ya kueleza sifa na kazi za Dk. Mengi, Spika Ndugai kuwa, Bunge limeungana na Rais John Magufuli kuomboleza kifo cha mfanyabiashara huyo ambaye pia aliyekuwa Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Media.
“Katika kuombeleza kifo na msiba huu mkubwa, sisi Bunge tunaungana na mheshimiwa Rais John Magufuli, familia ya marehemu na Watanzania wote kuomboleza na tukimshukuru Mungu,” amesema Spika Ndugai.
Spika Ndugai amesema, Bunge litaukumbuka mchango wa Dk. Mengi enzi za uhai wake, ikiwemo kusukuma gurudumu la maendeleo ya nchi kupitia sekta ya viwanda na tasnia ya habari.
Akielezea mchango wa Dk. Mengi kwa Taifa, Spika Ndugai amesema alikuwa mstari wa mbele katika kusaidia shughuli za ulinzi wa mazingira, pamoja na kusaidia watu wasiojiweza na wenye uhitaji.
“Tunamshukuru Dk. Mengi kwa mchango wake mkubwa usiopimika katika taifa hili, tutamkumbuka daima kwa jinsi alivyosaidia sana hifadhi ya mazingira hasa maeneo yanayozunguka Mlima Kilimanjaro kwa mamilioni bila kuchoka, alikuwa mmiliki wa vyombo vya habari na mmiliki wa viwanda kadhaa,” amesema Spika Ndugai na kuongeza;
“Na alikuwa kiongozi wa umma akiwa ni mwenyekiti wa bodi mbalimbali na mengine mengi ya binafsi. Pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Mazingira na Kamishna wa TACAIDS.”
Spika Ndugai amesema, katika maisha yake Dk. Mengi alipata tuzo nyingi za kitaifa na kimataifa, alijulikana kwa utoaji misaada ya kijamii, ujenzi wa misikiti, makanisa.
Pia alikuwa msaada kwa wasiojiweza ikiwemo walemavu wanyonge na kutoa tiba kwa wagonjwa mbalimbali hasa wa moyo.
Leave a comment