KLABU ya Soka ya Simba imeapa kuondoka na ushindi kwenye mchezo watani wa jadi wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Yanga kwa kuwa timu yao kwa sasa ipo vizuri. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo wa mzunguko wa kwanza, ambao Simba ndiyo watakuwa wenyeji utapigwa kwenye dimba la Benjamin Mkapa, tarehe 11, Novemba 2021 majira ya saa 11 jioni.
Akizungumza kwenye mkutano Mkuu wa mwaka wa klabu hiyo, uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mwalimu Nyerere, Mwenyekiti wa bodi ya klabu hiyo Salim Abdallah ‘Try Again’ amesema kuwa wanasimba kwa sasa wanakila sababu ya kutembea kifua mbele, kwa kuwa timu yao ipo kwenye mikono salama.
“Wanasimba mnakila sababu ya kutembea kifua mbele msiwe wanyonge, Simba ipo kwenyre mikono salama, watake wasitake mpira utachezwa mmeona juzi Mwanza, sisi ni Tik-taka tu,” alisema Try Again.
Aidha mwenyekiti huyo wa bodi, aliendelea kusema kuwa wao ndiyo wenyeji wa mchezo huo na aliwahakikishia wanachama hao kuwa wataifunga Yanga kwa kuwa mbinu zao zote wanazijua.
“Tarehe 11, mwezi ujao tunashughuli pale sisi ndio wenyeji nataka tuwahakikishieni tutawapiga, mipango yote tunaijua mbinu zote tunazijua,” aliongezea.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo alisema kuwa Simba kwa sasa imewekeza kwenye mpira na siyo kuwekeza kwenye vijembe kwa kuwa wao ni moja ya klabu 10 bora barani Afrika.
“Simba imewekeza kwenye mpira, Simba haijawekeza kwenye kejeri fitna na vijembe, huku tumeshapita, ndani ya klabu 10 bora Afrika Simba tumo hao wengine sijui ya ngapi,” alisema Try Again.
Leave a comment