WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Uwekezaji nchini Tanzania, Geoffrey Mwambe, amesema wizara yake iko hatua za mwisho kurekebisha Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya mwaka 1997, ili iende na wakati. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mwambe amesema hayo leo Jumatatu, tarehe 17 Mei 2021, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Mwambe amesema, kama mapitio ya sheria hiyo yatamalizika mapema, muswada wake utawasilishwa katika vikao vya Bunge, vinavyotarajiwa kuahirishwa Juni 2021.
“Lakini pia, mapitio ya sheria yako kwenye hatua za juu, na tunataka Mungu akijaalia kwenye bunge hili hili kabla ya halijaisha tarehe 30 Juni, tuwe tumeshafikisha bungeni,” amesema Mwambe.
Waziri huyo amesema, marekebisho hayo yanafanyika ili kuondoa mapungufu yaliyomo, ambayo yalikuwa yanarudisha nyuma maendeleo ya uwekezaji nchini.
“Ili kuboresha uwekezaji, tunahitaji tuwe na sera iliyokuwa nzuri ya uwekezaji, sera yetu ya uwekezaji ya 1996 ni ya siku nyingi sana ina miaka 25 sasa, na sheria yake mnaikumbuka Sheria ya Uwekezaji Tanzania Na. 26/1997, ni ya siku nyingi,” amesema Mwambe.
Waziri Mwambe amesema, amesema ” tumefanya fanya marekebisho katikati kidogo lakini bado haikidhi mahitaji, kwanza iko limited kwenye sekta ya uwekezaji, kuna sekta ambayo hatugusi ikiwemo sekta ya madini, petro lakini kemikali hatarishi.”
Ametaja upungufu uliyopo katika sheria hiyo kuwa, inayima mamlaka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), ya kusimamia masuala ya uwekezaji katika masuala ya gesi na madini.
“Kwamba sheria hii inasema TIC isiguse masuala hayo,kwa hiyo inapokuja uwekezaji kwenye LNG, Liganga na Mchuchuma, madini na miradi mengine, TIC haihusiki kwenye kupromote hilo eneo na kuwasajili.”
“Kwa sababu ni sekta imewekwa pembeni wakati wa uanzishaji viwanda ndio wanakuja TIC, kwa sasa mapitio ya sera yameshafanyika tuwe na sera mpya,” amesema Mwambe.
Waziri huyo amesema, “tunataka tuhakikishe kwamba madhaifu yote yaliyokuwepo kisheria ambayo yalikuwua yakifanya TIC isifanye majukumu yake vizuri, ikiwemo kuwahudumia wawekezaji, tuyabainishe mule na kufungua uwanda mpana wa sekta zote.”
Mwambe amesema katika marekebisho hayo, TIC itaanza kuwasajili wawekezaji wenye mitaji chini ya Dola za Marekani 100,000 kwa wazawa na 500,000 kwa wageni, ambao hawatambuliwi na sheria ya sasa.
“Hata namna ya kusajiliwa uwekezaji, sisi tunatoa cheti kimoja cha uwekezaji, ambacho kwa Mtanzania lazima uwe na mtaji usiopungua dola laki moja na kwa mtu wa nje usipoungua dola laki tano. Ukiwa na watu wenye mtaji chini ya hapo watakuja kuwekeza lakini haitakuja TIC,” amesema Mwambe na kuongeza:
“Kwa hiyo TIC haina kanzi data za taarifa za hao wote, kwa hiyo kwenye sheria mule tunataka tuweze kuwasajili wote. Tunataka kupitia sheria TIC iwe na mamlaka pamoja na wizara.”
Leave a comment