SERIKALI imesema jumla ya Sh66.86 bilioni zimekusanywa tangu kuanza kutoza tozo za kuvuka daraja la Kigamboni mwaka 2016. Anaripti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Ijumaa Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, akijibu swali la Mbunge wa Kigamboni, Faustine Ndungulile aliyetaka kujua kiasi kilichokusanywa hadi sasa katika daraja hilo.
Pia Ndungulile alitaka kujua mpango wa Serikali kufanya huduma za daraja hilo kuwa bure.
Akijibu swali hilo Kasekenya amesema kuwa Mfuko wa NSSF ulianza kupokea fedha zitokanazo na tozo kwa watumiaji wa Daraja la Nyerere mnamo tarehe 14 Mei, 2016 baada ya kuzinduliwa.
“Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei, 2022, Mfuko ulikuwa umekusanya jumla ya Shilingi Bilioni 66.86,” amesema.
Aidha amesema Serikali imeendelea kupunguza tozo kwa watumiaji wa Daraja hilo tangu kuzinduliwa kwake kwa kuzingatia tathmini ya uwezo wa wananchi kumudu tozo hizo.
“Kwa mara ya mwisho, Serikali imepunguza tozo husika tarehe 21 Mei, 2022,” amesema.
Leave a comment