SERIKALI ya Tanzania, imeweka mapingamizi manne katika kesi ya kikatiba, iliyofunguliwa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe akipinga utaratibu uliotumika kumkamata na kumfungulia mashtaka ya ugaidi katika mahakamani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Katika kesi hiyo, Mbowe amemshtaki Mwendesha Mashtaka wa Serikali (DPP), Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), akidai walikiuka katiba, ikiwemo katika taratibu walizotumia kumkamata akiwa jijini Mwanza na kumfungulia mashtaka pasina kumpa hali ya kuwa na wakili wake wakati wa mahojiano.
Leo Jumatatu tarehe 30 Agosti 2021, wakati kesi hiyo iliposikilizwa mbele ya Jaji John Mgetta, Wakili wa Serikali Mkuu, Hangi Chang’a, amesema Jamhuri imeamua kuweka mapingamizi manne, dhidi ya kesi hiyo.
Wakili Chang’a aliiomba mahakama hiyo isikilize mapingamizi hayo kwa njia ya maandishi.
Baada ya Wakili Chang’a kutoa ombi hilo, lililoafikiwa na upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili Peter Kibatala, Jaji Mgeta alipanga tarehe 6 Septemba 2021, kuwa siku ya upande wa Jamhuri kuwasilisha mapingamizi yao mahakamani hapo, kwa njia ya maandishi.
Pia, alipanga tarehe 9 Septemba 2021, kuwa siku ya upande wa utetezi kuwasilisha majibu yao dhidi ya mapingamizi hayo, kwa njia ya maandishi.
Jaji Mgetta aliipanga tarehe 23 Septemba 2021, kuwa siku ya mahakama hiyo kutoa uamuzi dhidi ya mapingamizi ya Jamhuri, kuhusu kesi hiyo iliyofunguliwa na Mbowe.
Mbowe amefungua kesi hiyo kupinga utaratibu uliotumiwa na Jeshi la Polisi mkoani Mwanza, kumkamata akiwa hotelini jijini humo, akijiandaa kushiriki kongamano la kudai katiba mpya lililoandaliwa na Chadema.
Pia, anapinga utaratibu uliotumika kumfungulia mashtaka ya ugaidi bila kumtaarifu kwa njia ya maandishi na kumwezesha kuwasiliana na wakili wake.
Leave a comment