WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imefuta pendekezo lake kuwapa wamachinga asilimia tano kati ya 10, ya fedha za mikopo inayotolewa na halmashauri kwa makundi maalum. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Mwigulu ameyasema hayo leo Ijumaa, tarehe 24 Juni 2022, bungeni jijini Dodoma, akijibu hoja za baadhi ya wabunge waliopinga pendekezo hilo, wakati wa mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2022/23.
Waziri huyo wa fedha amesema, Serikali imeamua kufuta pendekezo hilo lililowekwa katika bajeti kuu ya Serikali 2022/23, baada ya Rais Samia Suluhu Hassan, kusikiliza michango ya wabunge hao.
“Niwahakikishie Rais amefuatilia michango yenu, maelekezo aliyotupatia tulipopeleka mrejesho wa mjadala alisema wizara na wataalamu wasikilizeni wawakilishi wa wananchi. Kwa hiyo jambo hili limebaki vile vile,” amesema Dk. Mwigulu.
https://www.youtube.com/watch?v=kIF-uCefalY
Awali, Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Innocent Bashungwa, aliwahakikishia wabunge kwamba fedha hizo zitawafikia walengwa, huku akionya kuwachukulia hatua wakurugenzi wa halmashauri watakaoshindwa kusimamia vizuri mikopo hiyo.
“Tutaenda kuimarisha usimamizi wa fedha hizi kwa kutumia mifumo ya TEHAMA, lakini tunaenda kusimamia sheria kwamba wakurugenzi katika kutoa asilimia 10 sio hiari, bali ni takwa la kisheria. Lakini sambamba na hilo, nimeshaweka vigezo vya kuwapima wakurugenzi,” amesema Bashungwa na kuongeza:
“Moja ya vigezo vya kuwapima wakurugenzi ni kuangalia wanasimamiaje asilimia 10, kuzitoa kwa wakati kwenye asilimia 40 au 60 . Lakini kusimamia marejesho yake na kuzingatia utawala bora katika usimamizi wake.”
Leave a comment