AMIRI Jeshi Mkuu Rais Samia Suluhu Hassan, amewatunuku kamisheni wahitimu 62 wa Shahada ya kwanza Sayansi ya Kijeshi, pamoja na kuvunja mahafali ya nne ya shahada hiyo katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, jijini Arusha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya chuo hicho, leo tarehe 18 Novemba 2023, jijini Arusha.
Akizungumza baada ya kuwatunuku, Rais Samia amewataka maafisa hao kutumia mafunzo waliyopewa kuongeza weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
“Nishukuru uongozi wa Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi cha Monduli kwa kutoa mafunzo haya muhimu, nina imani kupitia mafunzo haya yatawaongezea maafisa wetu weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Rais Samia.
Awali, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, alisema wahitimu waliotunukiwa kamisheni hiyo, wanaume walikuwa 41 na wanawake 21.
“Chuo kinaendelea kutekeleza jukumu la kutoa mafunzo ya shahada ya kijeshi kwa kuzingatia matakwa ya kitaaluma na kijeshi.
“Aidha, chuo kinaendelea kufanya juhudi mahususi kuboresha mitaala na mafunzo hayo ili kuliwezesha jeshi na taifa kupata wahitimu wenye uwezo wa kupambana na wanaoweza kutatua changamoto mbalimbali za ulinzi kwa ustawi wa taifa letu,” amesema Mhandisi Masauni.
Leave a comment