RAIS Samia Suluhu Hassan amesema katika mikoa ya kusini mwa Tanzania kumeibuka ugonjwa wa ajabu ambapo watu wengi mfululizo wanavuja damu puani na kuanguka.
Pia amesema tayari timu ya wanasayansi na watalaam wa afya wametumwa kuelekea katika mikoa hiyo hususani Lindi kuchunguza aina hiyo ya ugonjwa ambao ameunasibisha kuwa unaweza kutokana na uharibifu wa mazingira. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea)
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 12 Julai, 2022 wakati akihutubia mkutano wa 20 wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati (AMECEA)
Mkutano huo unaofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 8 hadi 18 Julai mwaka huu, unaongozwa na kauli mbiu isemayo “Utunzaji wa Mazingira kwa Ajili ya Maendeleo Endelevu ya Binadamu.”
Aidha, Rais Samia akifafanua kuhusu maradhi hayo, amesema Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alimueleza kuhusu ugonjwa huo pindi alipofanya ziara katika mikoa ya kusini.
“Kuna maradhi ambayo huko nyuma hatuyajui, hayakuwepo lakini kwa sababu tunaharibika misituni, vile viumbe ambavyo vilipaswa vihifadhiwe kule msituni sasa vinasambaa kuja kwa binadamu.
“Kuna kila aina ya maradhi mapya yanazuka ambayo hatuyajui, nilikuwa nazungumza na waziri mkuu juzi ametoka ziara kule mikoa ya kusini Lindi ananiambia ameona kuna maradhi yameingia wanadamu wanatokwa tu damu za pua wanadondoka.
“Hatujui ni kitu gani wanasayansi, watalaam wa afya wote wamehamia huko wanaangalia ni kitu gani. Kwanini mwanadamu atokwe tu na damu za pua adondoke, angekuwa mmoja au wawili tungesema ni presha imepanda, vein zimebust anatokwa damu za pua lakini ni wengi kwa mfululizo, ni maradhi ambayo hatujawahi kuona na yote ni kwa sababu tunaharibu makazi ya viumbe kule walikoumbwa na Mungu tunawasogeza kwetu wanatuletea maradhi,” amesema Rais Samia.
Aidha, ametoa wito kwa waumini wa dini zote kwamba kuwa waangalifu na mazingira ili athari za uharibifu wake zisihatarishe mipango, maisha na maendeleo yao.
“Vilevile tutumie majukwaa yetu ya kiroho kuwahimiza waumini na wenyewe kutunza mazingira yao popote pale walipo. Nina hakika kuwa endapo tutasimama pamoja na tukasimama imara katika kusimamia mazingira yetu… tutafikia mustakabali mwema wa maisha na maendeleo ya mwanadamu,” amesema.
Leave a comment