MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini Tanzania (THRDC), umewataka waandishi wa habari kuibua matukio ya ukatili wa kijinsia hasusani kwa watoto, wanawake na watu wenye ulemavu ili mamlaka husika zichukue hatua kuyatokomeza. Anaripoti Regina Mkonde, Morogoro … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne, tarehe 12 Julai 2022 na Afisa Uchechemuzi wa THRDC, Wakili Nuru Maro, akiwasilisha mada katika mafunzo ya kuwajengea uwezo wanahabari katika kuripoti mienendo ya kesi na maamuzi ya mahakama pamoja na masuala yanayohusu haki za binadamu, yaliyofanyika mkoani Morogoro.
“Kama waandishi wa habari hawatavumbua maovu jamii haitajua lakini tunavyoibua tunatekeleza utetezi wa haki za binadamu kwa kutoa taarifa ambazo zitapekekea mamlaka husika katika eneo hilo ili kufanyiwa kazi,” amesema Wakili Nuru.
Wakili Nuru amesema, wanahabari wanapaswa kuibua matukio hayo ili kuhakikisha haki inatendeka kwani asilimia kubwa hayafikishwi mahakamani, yanatekelezwa na wanafamilia ambao huamua kuwaficha wahusika.
“Changamoto kubwa tunakuta kwenye mwitikio wa jamii, mfano kwenye masuala ya watoto tunaona kesi zinaenda mahakamani lakini ndugu wanashindwa kutoa ushahidi lakini watoto wananyanyaswa na wanafamilia mzazi anaona nikimpeleka mahakamani ndugu… jamii itanichukuliaje! Sisi wanahabari tuna jukumu la kubadilisha mtazamo huu,” amesema Wakili Nuru.
Aidha, Wakili Nuru amewaomba wanahabari kushirikiana na mashirika yanayotetea haki za binadamu, katika kufanya uchechemuzi juu ya maboresho ya sheria ambayo yatasaidia kupunguza au kutokomeza kabisa matukio hayo.
Katika hatua nyingine, Wakili Nuru amewaomba wanahabari kufuatilia mienendo ya kesi zinazohusu ukatili wa watoto ili kujua zinafikia wapi.
Leave a comment