RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemuagiza Inspekta Jenerali wa Polisi nchini humo (IGP), Simon Sirro, akomeshe vitendo vya uhalifu katika Mkoa wa Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametoa agizo hilo leo Ijumaa, tarehe 7 Mei 2021, katika Ukumbi wa Mlimani City mkoani Dar es Salaam, akizungumza na wazee wa mkoa huo.
Kiongozi huyo wa Tanzania, ametoa agizo hilo akisema, ameona taarifa za ongezeko la vitendo vya uhalifu katika mitandao ya kijamii.
“Nimesoma kwenye mitandao ya kijamii kwamba Dar es Salaam wanajaribu kina cha maji. Ujambazi na upokonyaji umeanza kuja juu, naomba nitoe meseji wasijaribu kina cha maji, IGP Sirro uko hapa, naomba ushughulikie,” amesema Rais Samia.
Sambamba na hilo, Rais Samia amesema, baadhi ya wananchi mkoani humo wanashauri kiongozi wa Jeshi la Polisi Dar es Salaam abadilishwe, aletwe mwingine na kumuagiza IGP Sirro asuhughulikie ushauri huo.
“Na katika mitandao ile wananchi wanasema alikuwuepo afande nani (hakumtaja jina), alikuwepo hapa wakasme mama turudishie, naomba hilo uliangalie vizuri,” amesema Rais Samia.
Kwa sasa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam inaongozwa na Lazaro Mambosasa, aliyeteuliwa na IGP Sirro Agosti 2017.
Mambosasa aliteuliwa kurithi mikona ya IGP Sirro, baada ya kamanda huyo kuteuliwa na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano wa Tanzania, Hayati John Magufuli, kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini humo.
Leave a comment