Mkuu wa mkoa wa Songwe Dk. Fransis Michael ameshangazwa na mienendo ya kesi zinazowahusu watu wanaodaiwa kuwapa ujauzito wanafunzi na kukatisha masomo yao, kwenda kwa kusuasua na kusisitiza adhabu zaidi itolewe kukomesha ‘mafataki’ hao. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe … (endelea).
Dk. Michael aliyasema hayo jana Jumatano kwenye kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa (RCC) mkoani humo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali na wadau wa taasisi mbalimbali.
Alisema serikali imetumia fedha nyingi kujenga shule ili watoto wasome na wawe viongozi wa baadae, lakini wapo vijana wanaojiita mabeberu wanaharibu na kukatisha ndoto za wanafunzi hao kwa kuwarubuni na kufanikiwa kuwapa ujauzito.
Alisema takwimu alizonazo ni kuwa watoto 60 waliopewa ujauzito, kesi zao zilipelekwa mahakamani lakini ni kesi mbili pekee zilizotolewa hukumu huku nyingine zikiwa hazijulikani hatma yake.
Alisema kutokana na kasi ya serikali kujenga, madarasa mapya na kuanzisha shule mpya sambamba na ujenzi wa mabweni ipo haja wadau kushirikiana kuwalinda watoto ili wasome shule bila kusumbuliwa na itolewe adhabu kali kwa mtu atakayebainika anamrubuni mtoto wa kike.
Aidha, Dk. Michael aliwaeleza wadau wakiwemo wabunge kujenga utamaduni wa kuwasomesha watoto wenye uhitaji maalum wakiwemo yatima ili waweze kumaliza masomo yao na kujiendeleza kimaisha kwani Mungu atawaoa thawabu kubwa.
Naye Mbunge wa Songwe, Philipo Mulugo (CCM) alisema tangu awe mbunge kwa zaidi ya miaka 10, amesomesha watoto 720 huku Mbunge wa Vwawa, Japhet Hasunga (CCM) akisema anasomesha watoto 60.
Matukio ya mimba za utotoni katika mkoa wa Songwe yamefikia asilimia 45 kitaifa na kuufanya mkoa huo ya kuongoza kwa matukio hayo yanayokatisha ndoto za wasichana kusoma
Leave a comment