MKUU wa Mkoa wa Dar es salaam, Amos Makalla, ameagiza wamiliki wa mabasi yaendayo mkoani, wafuate utaratibu wa kupakia na kushusha abiria katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Mbezi Luis. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Makalla ametoa agizo hilo leo Ijumaa, tarehe 9 Julai 2021, alipotembelea kituo hicho kilichopo wilayani Ubungo mkoani humo.
Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es Salaam, ameliagiza Jeshi la Polisi lisimamie utekelezwaji wa malekezo hayo.
“Hiki ndiyo kituo kikubwa cha mabasi, mimi kama mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama naagiza hiki ndio kituo unapoingia Dar es Salaam, mabasi yote yatapita hapa yatakuja katika kituo hiki Jeshi la Polisi lisimamie maelekezo haya,” amesema Makalla.
Makalla amesema Serikali inatambua kituo kimoja cha mabasi, hivyo hakuna maana kama kila mmiliki wa mabasi atakuwa na kituo chake cha kupakia na kushusha abiria.
Aidha, RC Makalla ameelekeza uongozi wa kituo hicho kuweka utaratibu wa baadhi ya mabasi kushusha abiria kwenye eneo la kulaza magari, ambalo lina mabanda ya mamalishe ili kuchochea biashara zao.
Leave a comment