KLABU ya Soka ya Yanga imepenga kwenda kufanya maandalizi (Pre Season) kwa ajili ya msimu ujao wa mashindano nchini Morroco, siku chache mara baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara, kwa msimu huu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Yanga ambayo msimu ujao itashiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika, kama ikifanikiwa kumaliza Ligi kwenye nafasi ya pili, kufuatia Tanzania kuingiza timu nne kwenye michuano hiyo.
Akizungumza akiwa njiani kuelekea nchini Morocco kwa ajili ya maandalizi ya kambi hiyo, Mkurugezni wa uwekezaji wa kampuni ya GSM na makamu Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya Yanga, Mhandisi Hersi Saidi amesema kuwa anakwenda nchini humo kuangalia miundombinu na taratibu zingine.
“Ninakwenda huko na nitatembelea klabu ya Raja Casablanca kwa ajili ya maandalizi ya kwenda kufanya Pre-Season nchini Morocco.”Alisema Hersi
Hersi ambaye alizungumza hayo akiwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Instabul, nchini Uturuki ambapo alikuwa akiunganisha ndege kwenda Morocco aliongezea licha ya kwenda kuangalia miundombimu ya klabu hiyo ya Raja Casablanca lakini pia atakuwa na mazungumzo na viongozi mbalimbali wa CAF, kutokana na kuwa na mkutano nchini humo, lakini pia kuangalia fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
“Pia nitafanya maongezi na viongozi mbalimbali wa CAF, kwa kuwa watakuwa na mkutano huku, na kaungalia fainali ya Ligi ya Mabingwa ambayo nimepata mualiko kutoka kwa rafiki zangu wa Kaizer Chiefs.” Aliongeza Hersi
Ikumbukwe Raja Casablanca na klabu ya Yanga, Aprili 21 mwaka huu walisaini mkataba wa mashirikiano katika sekta mbalimbali za kimaendeleo wakati timu hiyo ilipokuja nchini kucheza mchezo wa kombe la Shirikisho dhidi ya Namungo FC.
Klabu hiyo pia leo itamuaga aliyekuwa kiungo wao kwa misimu Zaidi ya nane, Haruna Niyonzima, kwenye dimba la Uwanja wa Benjamin Mkapa, ambapo Yanga itashuka Uwanjani dhidi ya Ihefu FC kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Sherehe hiyo itasindikizwa na wasanii mbalimbali ikiwemo Juma Nature, Shetta pamoja na Mzee wa Bwaksi.
Leave a comment